Na Lilian Lugakingira, Bukoba
UBORESHAJI wa elimu ya msingi na sekondari nchini utaweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa endapo wasomi kutoka katika fani mbalimbali, watakubali kurudi nyumbani kwao na kutoa misaada katika shule walizosomea.
Hayo yalisemwa na mfanyabiashara maarufu wa mjini Bukoba, Remigius Patrick, wakati wa hafla fupi ya kukabidhi msaada wa madawati 30 yenye thamani ya Sh900,000 kwa shule ya msingi Omukilembo iliyoko Kata ya Bugandika Wilaya ya Bukoba.
Patrick alisema endapo watu hao ambao ana uhakika kuwa wapo wenye uwezo mkubwa kifedha, watakumbuka kurudi kwao na kutoa misaada kama hiyo, wataweza kuondoa matatizo ya upungufu wa madawati shuleni, upungufu wa nyumba za walimu, vyumba vya madarasa na ujenzi wa vyoo.
Alisema misaada mingine pia ya sare za shule, viatu, madaftari, karo na mahitaji mengine muhimu ya shule pia nayo yanaweza kutatuliwa kwa njia hiyo hasa kwa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu.
Mfanyabiashara huyo ambaye pia ni mlezi wa shule hiyo alisema kuwa ameamua kutoa msaada huo kama njia mojawapo ya kulipa fadhira katika shule hiyo aliyosomea na kuwa msingi mzuri wa maisha na mafanikio aliyo nayo ni matunda ya shule hiyo.
Pia mfanyabiashara huyo, aliahidi kuwalipia karo na mahitaji yote ya shule kwa mwaka mmoja wanafunzi wote tisa, waliochaguliwa kuendelea na masomo katika shule mbalimbali za sekondari ili kuwawezesha kuendelea na masomo yao.
Awali akitoa taarifa ya shule hiyo Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Donatus Ishengoma alisema shule hiyo ina wanafunzi 332 na walimu nane na kuwa ina upungufu wa madawati 60, ambao alisema zinafanyika jitihada za kila namna ili kuhakikisha madawati hayo yanapatikana.