NA RASHID MUSSA, MTWARA
WAFANYAKAZI zaidi ya 3,000 wa kiwanda cha korosho cha Olam, mkoani hapa jana waligoma kufanya kazi na kuandamana hadi ofisi ya mkuu wa mkoa, wakidai nyongeza ya mshahara waliyoahidiwa Januari, mwaka huu. Kwa mujibu wa wafanyakazi hao, ambao baada ya kufika kazini jana asubuhi wote walitoka nje, walilalamikia nyongeza waliyopewa kuwa ni ndogo.
Walidai kuwa waliahidiwa kuwa mwezi huu wangeongezwa sh. 65 kwa kila kilo moja ya korosho wanayozalisha.
Wafanyakazi hao walidai badala ya kiwango hicho, wameongezwa sh. 10kwa kilo moja wanayozalisha; nyongeza ambayo wamedai ni ndogo mno sawa na kuwadhihaki kulingana na ugumu wa kazi, mazingira ya utendaji na kupanda kwa hali ya maisha.
Asilimia kubwa ya wafanyakazi hao hulipwa kulingana na uzalishaji wa kila mtu katika idara anayofanyia kazi.
Walidai kiwanda kinapata faida kubwa kwa mauzo ya mali wanayozalisha, ikizingatiwa kuwa wawekezaji katika viwanda vya korosho wamesamehewa ushuru kwa asilimia 10 wa mauzo ya nje.
Wauzaji wa korosho ghafi nje hutozwa ushuru wa asilimia 10.
Uongozi wa kiwanda haukuwa tayari kuzungumzia madai ya
wafanyakazi hao, ambao karibu asilimia 90 ni wanawake, kwa madai kuwa wasemaji ni menejimenti ya Olam makao makuu.
Hata hivyo, uongozi ulikiri kuwepo na makubaliano ya nyongeza ya malipo yao, lakini si ya kiwango wanachodai wafanyakazi. Ulidai kuwa ahadi hiyo
imetimizwa kwa kuongeza malipo yao kati ya sh. 10 hadi sh. 19 kulingana na kazi ya muhusika.
Uongozi huo umedai kuwa nyongeza hiyo imezingatia gharama za uzalishaji ambazo zimepanda kutokana na matatizo ya umeme na maji, na pia bei ya korosho katika soko la dunia kushuka.
Taarifa kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa ambako wafanyakazi hao walikutana na Ofisa Tawala wa mkoa, Hemed Matuwila zilisema wametakiwa kusubiri matokeo ya majadiliano ya maslahi yao yanayoendelea ya kamati maalumu iliyoundwa.