NA ELIZABETH MAONI, SUMBAWANGA
ASILIMIA 90 ya majengo ya shule za msingi na sekondari mkoani Rukwa, yamejengwa kwa kutozingatia vipimo na ramani vilivyotolewa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, imefahamika.
Hayo yalielezwa hivi karibuni na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, iliyotembelea mkoani Rukwa kukagua maendeleo ya elimu.
Akisoma majumuisho ya ziara ya kamati hiyo, Mwenyekiti wake Mbunge wa Iramba Mashariki, Mgana Msindai alisema majengo mengi hayajafuata vipimo na ramani inayokubalika, hali inayoonyesha kuwa wahandisi hawafiki katika maeneo ya vijijini kukagua ujenzi unavyoendelea.
Alisema wilaya ya Nkasi ndiyo inayoongoza kwa kuwa na majengo yaliyojengwa chini ya kiwango, hali iliyoilazimu kamati hiyo kuagiza baadhi ya majengo ya madarasa kubomolewa na kujengwa upya.
Msindai alisema Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga imejaribu kufanya vizuri.
Kamati hiyo imewataka wakurugenzi wa halmashauri zote za mkoa huu kutekeleza maagizo yanayotolewa, ili kurekebisha kasoro zilizojitokeza kabla ya Aprili, mwaka huu.
Agizo hilo lilitolewa kufuatia kamati hiyo kubaini taarifa za fedha zisizo sahihi za manunuzi ya vifaa vya hospitali ya wilaya ya Mpanda. Zilitofautiana na zilizotolewa awali.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Daniel ole Njoolay aliiomba kamati hiyo kuangalia uwezekano wa kukagua miradi ya maendeleo mkoani Rukwa kila mwaka, ili kuongeza kasi ya utekelezaji.