Na Samuel Msuya, Morogoro
KATIKA harakati za kudhibiti upataji mimba kwa wasichana wa shule za msingi, Mkuu wa Mkoa Morogoro, Meja Jenerali Mstaafu Said Kalembo ameagiza kuwa sasa anahitaji kuona idadi ya watuhumiwa waliokamatwa kwa kosa hilo na si idadi tu ya wasichana waliojazwa mimba.
Kalembo alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati wa kikao cha kujadili maendeleo mbalimbali ya mkoa huo, yaliyofanyika mjini hapo katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Oasis.
Alisema amechoka kusikia maneno ya kuwa wasichana kadhaa wametiwa mimba, hivyo kuwataka wahusika wa sheria waweze kuwachukulia hatua mara moja watuhumiwa wa matukio hayo ambao ni wanaume.
Alisema kuwa kitendo cha kusikia kuwa wasichana wamepewa mimba na watuhumiwa pasipo kuchukuliwa hatua, huchochea vitendo hivyo kuendelea kwani wengine nao huiga baada ya kuona wenzao hawajachukuliwa hatua zozote za kisheria.
Hata hivyo, Kalembo aliwaomba wazazi kuwaandikisha shule watoto wao mwaka huu na kusisitiza kuwa yeyote atakayebainika kutofanya hivyo atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Alisema wazazi ni lazima wahakikishe wanawaandikisha watoto wao na kuwafuatilia kama wanahudhuria masomo ili kudhibiti utoro.
Alisema utoro umekuwa ni sugu kwa baadhi ya watoto mkoani hapa, kutokana na baadhi ya wazazi kushindwa kuwafuatilia kama wanaenda shule na kuhudhuria vipindi.
Mkoa wa Morogoro una idadi kubwa ya washichana wanaopata mimba ambapo kwa mwaka jana, jumla ya wasichana 509 walishindwa kumaliza elimu ya msingi na kujiunga sekondari