Awamu ya Nne Tuutokomze Umasikini
Mimi kama Mtanzania na mzalendo naomba nitoe salaamu zangu za mwaka mpya wa 2007 kwa Watanzania wote popote walipo Duniani hasa walioko Tanzania. Ninayo furaha kubwa kuingia mwaka huu hasa kwa kuwa mvua nyingi zimeendelea kunyesha sehemu karibia zote za nchi yetu na mgawo wa umeme kuisha. Lakini pamoja na furaha yote hii bado kuna jambo ambalo linanisumbua sana katika akili yangu kila kukicha nalo ni jisi gani tuuondoe umasikini katika nchi yetu.
Ndugu zangu Watanzania Kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu. Ukweli ni kwamba tukiwezesha kilimo tutakomboa zaidi ya asilimia 80 ya watanzania wanaotegemea kilimo an tutaweza kuwatoa kutoka katika wimbi la umaskini uliokisiri. Ninachoomba Watanzania tukiongozwa hasa na Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika jambo hili la kuondoa umasikini tufanye mambo yafuatayo:-
- Tuuchukie umaskini kwa kumaanisha na tuamini kwamba tunaweza kuuondoa huu umaskini ulio katika maisha yetu. Pia tuamini kwamba umasikini ulio kwa jirani zetu ni umaskini wetu pia na tunaweza kusaidiana wote kwa pamoja katika kuuondoa huo umaskini.
- Tujiamini katika uwezo wetu tulionao Watanzania kwamba tukifunga mikanda kweli kweli tunaweza kumshinda huyu adui umasikini. Hii ninamaanisha kuwa tusiamini sana katika kuegemea misaada kutoka nje ya nchi na badala yake tuamini katika kutumia mali zetu kidogo tulizo nazo.
- Tujenge fikra za kiuzalendo zaidi wala siyo za kibepari maana ndani ya nchi twaweza kujikuta baadhi yetu tunaishi kupitia migongo ya wenzetu. Na hii itakuawa hatari zaidi kwa maana hata yule mkoloni wakati baba zetu walikuwa wakipigania uhuru moja ya mambo yaliyowakasirisha ni kwa mkoloni kuishi kwa kupitia jasho lao. Sasa naomba tusije tukafikia hali hiyo tukasababsha watu tukaanza kudai uhuru mwingine ndani ya taifa moja lililo huru.
- Ndugu wananchi naomba tuamini kuwa tukitaka maendeleo na kuusahau umasikini wetu lazima kwanza kuna kujinyima, kuvumilia matatizo tutakayoyapata na kufanya kazi kwa bidii zaidi.
- Tuweke malengo ya kila kazi tutayokuwa tukiifanya katika kilimo na tutumie wataalamu wachache tulionao katika kuendeleza kilimo bora.
Kama tunataka tubadilishe hishoria ya nchi hii kweli badala ya kuwa nchi iliyo na watu masikini wa kupindukia iwe ni nchi yenye watu wenye maisha bora ninalo ombi na ushauri wa pekee kwa Mheshimiwa Rais kwamba:-
- Atoe tamko rasmi kuwa Umasikini ndiyo adui wetu nambari moja wa taifa letu la Tanzainia
- Kwa kuwa yeye Rais ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa majeshi yetu ya ulinzi na usalama atoe tamko la kumsaka huyu adui Umasikini popote pale alipo na akamatwe. Hii ninamaanisha kuwa askari wetu wawepo katika kila kijiji katika nchi yetu
- wakiangalia mwenendo mzima wa kilimo hasa wakati huu mvua zikiendelea kunyesha.
Watahakikisha kuwa kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanye kazi pasiwepo mtu wa kuzurura zurura bila kazi yoyote. Mimi binafsi sina shaka na wanajeshi wetu, kwamba watamkamata tu huyu adui umasikini na Watanzania tutafurahi na kujivunia Jeshi letu. Ninaamini kuwa wanajeshi wetu wanaweza, hakuna linaloshindikana kwao na watatufanya tulime kwa bidii zaidi na tutapata mazao mengi zaidi.
Kila mwanachi au kaya itatakiwa kupangiwa kiwango chake cha shamba na kuhakikisha linatunzwa vizuri likifuata njia sahihi za kitaalam ambazo zitatolewa na Bwana shamba ambao wapo kila kijiji na ni lazima nao wawajibike katika kazi zao ipasavyo. Kila familia naamini itafurahi kwa kupata mazao mengi na kuepukana na balaa la njaa na pia tutaweza kuuza mazao yetu na kuweza kuboresha maisha yetu hasa nyumba zetu za vijijini. Tutaweza kujenga nyumba za kudumu na barabara zetu za vijiji tutaziimarisha kwa kushirikiana wote kwa pamoja tukipata maelekezo sahihi kutoka kwa wataaalamu wetu wachache tulionao.
- Atoe tangazo kwa Watanzania wote kwamba sasa tuko vitani dhidi ya Umasikini na kwamba kilimo ndiyo njia pekee itakayotuwezesha kumuondoa huyu adui.
- Atoe tamko kwa Watanzania wote waishio mijini asiwepo mtu yeyote mwenye uwezo wa kufanya kazi aishi mjini bila kazi iliyo rasmi ya kufanya bali aende katika kijiji chochote atakachochagua yeye na atapewa eneo la kulima.
Ndugu zangu mimi ninakerwa sana kila ninapokutana na taarifa au maandishi yanayosema Tanzania is one of the poorest countries in the world, sijui nyie wenzangu mnajisikiaje na hili maana naamini mmekutana nayo mara nyingi sana. Mawaziri, Watumishi wa umma, Wabunge, Wafanyabiashara na watumishi katika makampuni binafsi na wananchi wote kwa ujumla sasa basi tuungane pamoja kila mmoja alichukie hilo neno maana ni baya na tujenge nchi yetu.
Kinachotakiwa hapa ni jambo moja tu tufanye kazi kwa ubunifu wa wastani unaozingatia mwenendo na hali ya nchi yetu. Maana kuna ubunifu unaolenga nchi za ulimwengu wa kwanza ambao unahitaji fedha nyingi ambazo sisi hatuna na hii ndiyo inyotupelekea kwenye kuomba misaada na kuingia katika madeni makubwa kabisa yasiyo ya lazima. Ubunifu wa maendeleo yoyote uzingatie zaidi uwezo wa ndani.
Kwa mfano tunapotaka kupima viwanja vijijini ili watu waweze kuishi kwa mpangilio unaojali upatikanaji wa huduma za muhimu kama barabara hatuhitaji fedha nyingi sana za kukopa bali kijiji kipewe dhamana ya kupima viwanja katika maeneo yake kama ni kwa kunyoosha kamba sawa ili tuishi katika maisha yanayozingatia huduma muhimu na mpangilio mzuri.
Siamini wananchi wa Tanzania hii tulioko vijijini tusiweze hata kunyoosha mitaa yetu wenyewe kwa vipimo vyenye hesabu ndogo bali unahitajika usimamizi na mamlaka. Huo ni mfano tu mmoja lakini ipo mingine mingi inayofanana na hiyo. Na kwa watafiti wetu hasa vyuo vikuu tafiti zote zizingatie mazingira, uwezo wa wananchi na umuhimu wake kwa sasa.
Maoni yangu tutoe kipaombele kwa tafiti zinazohusu kilimo na afya. Tusianze tafiti za kuunda na kurusha ndege au roketi angani, hizi zote zitakuja baada ya kuwa tumejenga uwezo wetu wa ndani. Hivyo basi kila Kijiji:
- Kitabuni mipango yake madhubuti ya kuleta ufanisi katika kilimo ikiwa ni pamoja na kujiwekea malengo ya kisai cha eneo ambalo kwa wastani kila mwanachi anaweza kulima, kuorodhesha mazao makuu yanayostawi katika eneo husika, kutoa aina ya mbolea inayofaa katika eneo husika na kutumia mbegu bora.
- Kitatoa taarifa ya kiasi ambacho mwanchi anaweza kutumia kama chakula kwa mwaka
- Kitabuni mipango ya pamoja dhidi ya uhifadhi wa mazao kitaalamu na kitapanga mikakati ya utafutaji wa masoko ya mazao yao ndani na nje ya nchi.Baada ya kuwa na uhakika wa chakula katika vijiji vyetu ndipo viwanda vidogovidogo vitaanza kwa kusindika baadhi ya mazao yetu ili tuuze yakiwa katika viwango ambavyo vitaleta pesa nyingi zaidi na ndipo uchumi wetu utaanza kukua.