Rais Jakaya Kikwete amewaondoa hofu wanachama wa mifuko minne ya hifadhi ya jamii kuwa fedha zilizotumika kujengea jengo jipya la Bunge mjini Dodoma, zitalipwa kama walivyokubaliana.
Mashirika yaliyochangia katika ujenzi wa jengo hilo lenye uwezo wa kubeba watu 800, ni Mfuko wa Hifadhi ya Jamii, NSSF, Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Serikali za Mitaa, LAPF, Mfuko wa Pesheni wa Watumishi wa Serikali Kuu,PSPF na Mfuko wa Watumishi wa Mashirika ya Jamii,PPF.
Jengo hilo ambalo ni la tatu kwa ubora na ukubwa barani Afrika limetafuna Sh. Bilioni 30 ikiwa ni gharama ya ujenzi, vifaa mbalimbali vya mawasiliano na usalama pamoja na samani.
Rais aliyasema hayo mjini hapa jna wakati akifungua jengo jipya la bunge ambalo limeanza kutumika leo katika kikao cha bajeti.
Alisema yeye na wenzake Serikalini wanajua kuwa wametumia fedha za wanachama wao na wakati ukifika inabidi kulipa deni.
Alisema bunge hilo ni kiota cha mijadala muhimu ya kitaifa, mijadala itakayoamua mwelekeo wa demokrasia, hatma ya maendeleo na mustakabali wa taifa la Tanzania.