Na Brandy Nelson, Mbeya
WAZIRI wa Afya na Ustawi wa Jamii, Profesa David Mwakyusa amesema sheria iliyounda Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya inatakiwa kufanyiwa mapendekezo ya marekebisho ya haraka ili makundi zaidi katika jamii yaweze kunufaika.
Aliyasema hayo jana alipokuwa akifungua siku ya wadau wa Mfuko huo, mkoani wa Mbeya, kwenye Ukumbi wa Benjamini Mkapa, jijini hapa.
Alisema kwa sasa watu walio nje ya utaratibu huo wanapata tabu kugharamia matibabu yanayopanda kila wakati, hivyo kuwafanya kuwa na hofu juu ya maisha yao wanapougua au kuuguliwa.
“Hakikisheni watanzania wengi wananufaika na huduma za Bima ya Afya na kazi hii ifanywe kwa ushirkiano kati ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na ile ya Afya ya Jamii, ili tukifika mwisho wa mwaka huu tuwanufaisha angalau asilimia saba ya watanzania wote,” alisema.
Profesa Mwakyusa alisema suala la huduma bora ni muhimu, hivyo jambo hilo lizingatiwe na watoa huduma kwa sababu huwavuta wateja na huduma mbovu huwafukuza.
“Ni vyema tujiulize kama huduma ambazo zinatolewa na vituo vya matibabu kwa wanachama wa mfuko huu zina ubora wa kiwango gani? Lengo lenu kama watoa huduma liwe ni huduma bora isiyo na bugudha kwa wagonjwa,” alisisitiza Profesa Mwakyusa.
Alisema kila mmoja atafakari kama wagonjwa anaowatibu kituoni kwake wanakwenda pale kwa kukichagua kituo hicho au kwa sababu hawana sehemu nyinge mbadala.
Awali, Mkurugenzi wa Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Emanuel Humba alisema lengo la siku ya wadau ni kupata mrejesho kuhusu utekelezaji wa shughuli za mfuko na kupata maoni ya wadau katika maeneo mbali mbali.
Humba alisema uzoefu walioupata mwaka 2006/2007 ni kwamba katika kila mkoa kuna wilaya moja au zaidi zenye uhaba wa vituo ambavyo pia vinamtandao hafifu ikilinganishwa na wilaya nyingine katika mkoa husika.
Alizitaja wilaya na hizo na mikoa kwenye mabano, kuwa ni Liwale (Lindi), Rufiji (Pwani), Temeke (Da es salaam), Chunya na Mbarali (Mbeya), Masasi (Mtwara), Kondoa (Dodoma) na Manyoni (Singida).