Na Maimuna Kubegeya
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini-Chadema, Zitto Kabwe, jana alihojiwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusiana na madai kuwa alitoroka vikao vya Bunge na kwenda sarafini Ujerumani na kutoa matamshi ya kumdharau Spika wa Bunge.
Kikao cha kamati hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Juma Nh'unga kilifanyika jana katika Ofisi ya Bunge jijini Dar es Salaam ambako Kabwe aliitwa kuhojiwa na kujitetea kuhusiana na tuhuma hizo.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Wilson Masilingi, (Muleba Kusini-CCM) alithibisha kuwapo kwa kikao hicho na akasema kuwa kisheria kikao hicho huwa ni cha ndani na yanayojadiliwa huwawasilishwa kwa Spika wa Bunge la Muungano.
Mwenyekiti Nh'unga alipoulizwa kwa njia ya simu kuhusiana na kikao hicho na agenda zake, alikataa kuzungumzia suala hilo kwa maelezo kwamba yeye si msemaji na kutaka gazeti hili liwasiliane na Spika wa Bunge, Samuel Sitta.
Hata hivyo baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo walithibitishwa kufanyika kwa mkutano huo na kuwa moja ya agenda ilikuwa suala la Kabwe.
Chanzo cha habari kilisema kuwa Kabwe alitakiwa kutoa maelezo ni kwa nini alitoroka bunge na kwenda Ujerumani na matamshi yake aliyoyatoa kwa vyombo vya habari Novemba 2, mwaka jana kuhusiana na uelewa mdogo wa Sitta kuhusiana na kanuni za Bunge na kushindwa kuomba kuomba radhi kwa muda wa siku tano alizopewa na Spika.
Hata hivyo baadhi ya wajumbe hao hawakuwa tayari kueleza maamuzi yaliyofikiwa na kamati hiyo, zaidi ya kueleza kuwa taarifa ya kamati hiyo inapelekwa kwa spika wabunge.
Mapema kabla ya kuingia katika kikao hicho, Kabwe alithibitisha kuitwa na kamati hiyo kwa barua ya Januari 6, mwaka huu ili kujibu tuhuma zinazomkabili.
Hata hivyo Kabwe alisema kwamba hajawahi kumdharau Spika Sitta na kuwa anauheshimu mchango anautoa katika bunge na hasa kwa wabunge vijana kama yeye kutokana na uzoefu alionao.
Alisema chama chake kimemteua Halima Mdee mbunge wa viti maalum kupitia Chadema kumpa msaada wa kisheria pindi utakapohitajika wakati wa kikao hicho.
Lakini habari kutoka ndani ya kikao hicho, zilisema kuwa Mdee hakuruhusiwa kuingia kwani haukuonekana umuhimu wa kuwa na msaada wa kisheria.