Kitaifa
   Siasa
   Jamii
   Uchumi
   Makala

 

Search


Advanced Search

 »  Home  »  Habari za Kitaifa  »  Migiro tayari kwa changamoto mpya UN
Migiro tayari kwa changamoto mpya UN
By Habari Tanzania | Published  01/9/2007 | Habari za Kitaifa | Rating:

Waandishi Wetu na Mashirika ya Habari

WAKATI Watanzania wakishangilia kuteuliwa kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Asha-Rose Migiro, kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), bosi wake mpya amewataka maafisa wa juu wa mashirika ya umoja huo kuandika barua za kujiuzulu.

Watu wanaotakiwa kujiuzulu ni pamoja na wakuu wa mashirika na taasisi mbalimbali za Umoja wa Mataifa pamoja na maafisa wengine wa ngazi za juu katika Umoja huo.

Ukiondoa Dk Migiro, katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-Moon, pia amemtua raia wa Mexico, Alicia Barcena, kuwa Katibu Mkuu Msaidizi wa Utawala katika umoja huo, uteuzi ambao hata hivyo umepokewa kwa wasiwasi na baadhi ya wawakilishi wa nchi katika umoja huo, wakisema hana uzoefu katika kusimamia mambo ya fedha.

Watu wanaotakiwa kuandika barua za kujiuzulu ni makatibu wasaidizi wote wanaosimamia taasisi na mashirika mbalimbali katika umoja huo ambao idadi yao inafikia 60.

Hata hivyo wale ambao uteuzi wao unasimamiwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na wale ambao uteuzi wao unatakiwa kufanyika baada ya mawasiliano na nchi wanazotoka, hawataguswa na operesheni hiyo.

Hata hivyo, Moon anasema kuwa si wote watakaondika barua za kujiuzulu watawekwa pembeni, bali amefanya hivyo ili kumpa nafasi ya kuunda timu yake ya utendaji kwa ajili ya kukabiliana na changamoto zinazoukabili umoja huo katika kipindi hiki.

Wakati huo huo, Dk Migiro, amesema taarifa za uteuzi wake kushika nafasi hiyo zilimshtua kwa kuwa hakuwahi kutarajia kupewa dhamana kubwa kiasi hicho maishani mwake.

"Nilishtuka nilipopata taarifa, sikuwa nimetarajia, ni dhamana kubwa niliyopewa, ila nimeipokea dhamana hii kwa unyenyekevu mkubwa," alisema.

Akizungumza katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, akitokea Maseru, Lesotho, jana, Dk Migiro alisema moja ya mambo makubwa anayotarajia kukabiliana nayo ni changamoto iliyopo sasa duniani, ya kuwapo masuala yanayohatarisha amani ya dunia.

"Ninapoichukulia picha ya jumla kwa sasa tunakabiliwa na changamoto kubwa ya kuhakikisha tunaimarisha amani na usalama, mambo ambayo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameshasema kuwa anayapa umuhimu wa kipekee, ninaamini tutaweza kutekeleza majukumu yetu vizuri zaidi," alisema.

Katika mapokezi hayo ambayo yalizua tafrani baada ya wanandugu, wanachama wa CCM, waliokuwa wafanyakazi wenzake katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na wanahabari kumzonga, hatua iliyomsababisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro kuingilia kati ili kutuliza hali hiyo.

Mapokezi hayo yaliyoongozwa na Kandoro, yalihudhuriwa pia na Mawaziri na naibu mawaziri wanawake, wakiwemo Waziri wa Fedha Zakia Meghji, Waziri wa Sheria na Katiba Dk Mary Nagu; Waziri wa Utumishi na Menejimenti ya Umma, Hawa Ghasia; Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rita Mlaki na Naibu Waziri wa Miundombinu Maua Daftari.

Wengine ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Kapteni Jaka Mwambi, Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Kapteni John Barongo; Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma, Matson Chizi; Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Patrick Tsere na viongozi wengine wa CCM na Serikali.

Dk Migiro aliteuliwa Januari 5, mwaka huu kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UN, wadhifa ulioanzishwa rasmi mwaka 1997 na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa chini ya uongozi wa Katibu Mkuu Kofi Annan, kama sehemu ya mabadiliko ya UN kwa ajili ya kusaidia shughuli za kiutawala za umoja huo.

Dk Migiro anashika wadhifa huo akiwa ni mtu wa tatu na mwanamke wa pili tangu nafasi hiyo ianzishwe.

Kwa mara ya kwanza wadhifa huo ulishikwa na mwanamke, Louise Fréchette, raia wa Canada aliyeanza kazi Machi 2, 1998 hadi Machi 31, mwaka jana.

Machi 3 mwaka jana, Mark Malloch Brown wa Uingereza, aliteuliwa kushika wadhifa huo na alianza kazi rasmi Aprili mosi hadi Desemba mwaka jana alipomaliza muda wake pamoja na Katibu Mkuu aliyepita, Kofi Annan.

Kazi za Migiro na wale waliomtanguliwa ni kumsaidia Katibu Mkuu katika kazi za kila siku za kuongoza sekretarieti ya UN.

Nyingine ni kukaimu nafasi ya Katibu Mkuu Makao Makuu ya UN, punde ikitokea hayupo, lakini pia anaweza kukaimu nafasi hiyo kama ataelekezwa kufanya hivyo na bosi wake.

Vile vile atamsaidia Katibu Mkuu kuhakikisha kunakuwapo na ufanisi katika shughuli mbalimbali za kisekta na taasisi za umoja huo, kuimarisha umoja na kusaidia maendeleo ya sera.

Jukumu jingine ni kumwakilisha Katibu Mkuu katika mikutano, matukio ya kiofisi yanayohusu umoja, sherehe na majukumu mengine kama itakavyoamuliwa na bosi wake na kupokea taarifa zinamzohusu Katibu Mkuu na ambazo atapaswa kuzishughulikia.

Akijibu maswali ya waandishi wa habari uwanjani hapo jana, Dk Migiro alisema ataendelea kupigania sera ya Umoja wa Mataifa kuhakikisha kuwa serikali zote duniani zinafuta adhabu ya kifo kwa kuwa adhabu hiyo inakwenda kinyume cha matakwa ya UN katika kulinda haki na uhuru wa binadamu.

Alisema anaamini kuwa kwa kushirikiana na watendaji wenzake ataendelea kusimamia misingi ya umoja, amani na mshikamano iliyomjenga tokea utotoni kupitia sera zilizowekwa na serikali zote zilizopita ambazo zimejenga mtazamo ulio sahihi kwake juu ya kulinda utu wa mwanadamu.

"Dira yangu ni misingi hii iliyonijenga tangu nilipokuwa nikikua, hadi nilipokuwa mtu mzima nilikuwa nikiamini katika misingi ya umoja, upendo na kuheshimiana kama misingi ya utu, lakini pia nimeweza kufahamu matatizo na masuala mbalimbali ya kimataifa na hasa nilipopewa dhamana na serikali yangu kuwa Waziri wa Mambo ya Nje, nitafanya kazi kwa kujituma," alisema.

Aliongeza kuwa katika masuala ya kimataifa ataendelea kuilinda dhamana ya Tanzania kwa kuhakikisha kuwa anaendeleza sera nzuri ya Serikali yake katika masuala ya Kimataifa, hasa katika kuhakikisha amani inapatikana katika nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Alisema akiwa mmoja wa watu wanaojua vyema matatizo ya umaskini yanatolikabili eneo hilo la Afrika, hasa kwa nchi zilizo Kusini mwa Jangwa hilo, atatumia nafasi yake kuhakikisha anafanya kila linalowezekana kukabiliana na hali ya watu wa huko.

"Nimezaliwa, nimelelewa na kukulia katika vijiji vilivyopo katika eneo hili, ninayafahamu vizuri mazingira yaliyopo, ninafahamu vizuri umaskini unaowakabili watu waliopo huku, ufahamu wangu huu utaniwezesha kuangalia namna ya kuzisaidia nchi hizi ziweze kukua kiuchumu," alisema.

Dk Migiro aliahidi kuwa atahakikisha anarejea nyumbani baada ya ukomo wa wadhifa wake huo ili aweze kuendelea kushiriki katika kutekeleza majukumu mbalimbali aliyokuwa nayo katika kuijenga jamii yake.

Baada ya mapekezi hayo, Dk Migiro alikwenda Ikulu kuzungumza na Rais Kikwete na baadaye kuhudhuria hafla ya kumpongeza katika Ofisi Ndogo za Chama Cha Mapinduzi (CCM) Lumumba.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dk Migiro aliwataka wana-CCM kukiimarisha chama na kudumisha uadilifu katika kipindi hiki ambacho chama kinajipanga kwa ajili ya kufanya uchaguzi mkuu.

Alisema mafanikio aliyoyapata na wanayoyapata Watanzania, yametokana na malezi mema aliyoyapata kuanzia katika Umoja wa Vijana wa Chama cha TANU (TANU Youth League), TANU hadi CCM.

"Bila malezi mema TANU Youth League, TANU hadi CCM, yametujenga Watanzania na ndio yamenipa sifa nzuri ya kuaminika," alisema Dk Migiro.

Alisema pamoja na kwenda kufanya kazi katika mazingira ya ugenini, ataendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa sera, ilani ya uchaguzi na ahadi zote ambazo chama kiliwaahidi wananchi katika kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka juzi.


How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent
Add comment
Comments


Article Options
Your Favorite Articles
View All Favorites
Articles to Read
You Recently Viewed...
Popular Articles
  1. Unaifahamu Jambo Forums?
  2. Barua ya Wazi kwa Rais Jakaya Kikwete
  3. Ghorofa Jijini lanusurika kuungua moto
  4. Is Tanzania a safe place to invest?
  5. Britsh M.P. calls for the suspension of aid to Tanzania.
No popular articles found.
Popular Authors
  1. Habari Tanzania
  2. Mzee Mwanakijiji
  3. Marshy Abdu
  4. Linda Garner
  5. Nthelezi Nesaa
  6. Prosper Kwigize
  7. Ramadhan Semtawa
  8. Salehe Mmoro
  9. Manyerere Jackton
  10. Ndesanjo Macha
No popular authors found.