Na Burhani Yakub, Tanga JESHI la Polisi Mkoani hapa limeagizwa kuendesha msako wa duka hadi duka hatimaye kukamata dawa za kulevya aina ya kuber ambazo zimekuwa zikiuzwa kana kwamba bidhaa hiyo ni halali.
Amri hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mohamed Abdulaziz alipokuwa akizungumza na wananchi katika sherehe za kuukaribisha mwaka 2007 zilizofanyika Hoteli ya Mkonge jijini hapa.
Alisema anashangazwa kusikia kuwa dawa hizo zimekuwa zikiuzwa kwenye maduka yaliyopo mkoani hapa hususani Jiji la Tanga na hakuna hatua zozote za kudhibiti zinzochukuliwa na vyombo vya dola kana kwamba hizo sia dawa za kulevya.
“Dawa za Kuber zinauzwa madukani bila aibu hii ni kashfa kwa serikali na nachukua fursa hii kuliagiza Jeshi la Polisi kuhakikisha linaendesha msako wa duka hadi duka na kuwachukulia hatua wanaoendelea kuendesha biashara hiyo haramu,” alisema Abdulaziz.
Akizungumzia dawa nyingine za kulevya mkuu huyo wa mkoa alieleza kusikitishwa kwake na vitendo vya baadhi ya watu wanaoiharibia sifa Tanga kwa kuifanya ni lango la kuingizia dawa hizo kutoka nje ya nchi.
Alitoa takwimu na kubainisha kuwa katika kipindi cha mwaka 2006 dawa aina ya Cocaine ilikamatwa ya uzito wa gramu 50.7, heroine gramu 69.2 wakati bangi jumla ya gramu 919 zilinaswa na ekari 18 na nusu za mashamba ya bangi ziliharibiwa na Jeshi la Polisi huku tani 10.2 zikiwa zimeteketezwa.
“Naagiza Poilsi Pamoja na wananchi waongeze juhudi katika vita hii kwa kufanya miskao na kuwakamata watu wote wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya mkoani kwetu”alisema Abduaziz.
Kuhusu matukio ya uhalifu Mkuu huyo wa Mkoa alisema mwaka 2006 yalipungua na kuwa 2034 ikilinganishwa na yaliyotokea 2005 ambapo yalifanyika 2240 ikiwa ni asilimia 9.2 na kwamba silaha kama SMG,Shotguns, Rifles na bastola zilikamatwa 98 huku risasi zikiwa 179.
Alisema mafunzo ya mgambo kwa mwaka 2006 yaliongezeka hadi kufikia 1022 tofauti na mwaka uliopita ambapo vijana waliopewa kutoka maeneo mbalimbali yakiwamo ya vijijini ni 852