Na Muhibu Said
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, kimeandaa mapokezi makubwa ya aina yake kwa ajili Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dk Asha-Rose Migiro, yatakayoambatana na sherehe za kumpongeza kwa kuteuliwa kwake kushika wadhifa huo.
Pamoja na wanachama wa chama hicho kutakiwa kujitokeza kwa maelfu katika Uwanja wa Ndege wa KImataifa wa Mwalimu Nyerere leo mchana, chama hicho pia kimepanga kumsindikiza kwa mbwembwe hadi Ikulu atakokuwa na mazungumzo mafupi na Rais Jakaya Kikwete.
Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, aliyekuwa Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Matson Chizi, alisema Dk Migiro, aliyeteuliwa na Katibu Mkuu mpya wa UN, Ban-Kin Moon Ijumaa wiki iliyopita kushika wadhifa huo, anatarajiwa kuwasili leo mchana akitokea Afrika Kusini. Migiro alikuwa katika ziara ya kikazi Lesotho, alipoteuliwa kushika wadhifa huo mpya.
Chizi amehamishiwa Dodoma na John Barongo ameteuliwa kushika nafasi hiyo.
Chizi alisema mapokezi hayo yatafanyika leo saa 8.40 mchana katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere na yataongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Jaka Mwambi.
Alisema mapokezi hayo yatafuatiwa na sherehe kubwa zitakazofanyika katika Ofisi Ndogo za CCM, barabara ya Lumumba, jijini Dar es Salaam, zitakazoanza saa 10.25 alasiri.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa jana na CCM Mkoa, mapokezi hayo yatapambwa na burudani zitakazotolewa na vikundi mbalimbali vya burudani kuanzia saa 6.30 mchana katika uwanja huo.
Pia bendi maarufu za muziki wa dansi nchini, ikiwamo Msondo Ngoma Jazz Band, TOT Plus na DDC Mlimani Park, zinatarajiwa kutumbuiza katika sherehe hizo.
Viongozi mbalimbali wa Chama Cha Mapinduzi na serikali wa ngazi za mkoa na kitaifa, pia watahudhuria katika mapokezi na sherehe hizo.
Chizi alisema baada ya Dk Migiro kuwasili uwanjani hapo, msafara wake utaondoka moja kwa moja kuelekea Ikulu ambako utapokelewa na Rais Jakaya Kikwete ambaye atafanya mazungumzo mafupi na Dk Migiro.
Alisema baadaye msafara huo utaondoka Ikulu na kuelekea Ofisi Ndogo za CCM, barabara ya Lumumba ambako utapokelewa na Katibu Mkuu wa Chama hicho, Yusuf Makamba.
Katibu huyo, alisema akiwa katika ofisi hizo, Dk Migiro ambaye pia ni Katibu wa Idara ya Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa wa CCM, atatambulishwa, kuwasalimu na kupokea salamu kutoka kwa wana-CCM na wananchi.
Pia atapewa zawadi kutoka CCM na Jumuiya ya Wanawake wa chama hicho (UWT) na baadaye atazungumza na Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya chama hicho (NEC-CCM) Taifa.
Kutokana na hali hiyo, Chizi aliwataka wana-CCM na wananchi wengine kujitokeza kwa wingi katika mapokezi hayo ili kuonyesha uzalendo wao kwa Dk Migiro.
Pia aliwataka viongozi, wanachama na wafuasi wa vyama vya upinzani kuhudhuria katika mapokezi na sherehe hizo akisema kwamba kuteuliwa kwa Dk Migiro kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UN, hakuwaletei sifa nzuri wana-CCM peke yake, bali Watanzania wote.
"Kuteuliwa kwake (Dk Migiro), kunaonyesha kuwa utawala ni mzuri, unapigania haki za binadamu na kuwatetea wanyonge, ameleta heshima kubwa kwa nchi," alisema Chizi