Zikiwa ni siku nne tu tangu basi dogo lililojaza watu kupita kiasi kutumbukia mtoni na kuua watu 54, basi lingine limepinduka na kuua nje kidogo ya mji wa Arusha.
Basi la Mtei Expres lenye namba za usajili T276 ADH lililokuwa likitokea Singida lilipinduka baada ya kugongana na gari dogo la aina ya LandCruiser.
WATU watatu wamefariki dunia papo hapo na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Bw. Basilio Matei alisema jana mjini hapa kuwa ajali hiyo ilitokea katika eneo liitwalo Tisongo.
Kwa mujibu wa Kamanda Matei, basi hilo lenye namba za usajili T276 ADH lilikuwa likitoka Singida kuja jijini hapa.
Alisema, lilipofika katika eneo hilo la Tisongo liligongana na gari dogo aina ya Land Cruiser lenye namba za usajili T362 AJW na kusababisha vifo hivyo.
Aidha, Kamanda huyo alisema kuwa uchunguzi wa ajali hiyo unaendelea na kwamba idadi ya waliojeruhiwa, majina yao pamoja na yale ya marehemu bado hayajafahamika.
Hata hivyo, watu walioshuhudia ajali hiyo walisema ilitokea baada ya dereva wa gari dogo kuyumba alipokuwa akiendesha huku akiongea kwa simu, jambo lililosababisha Land Cruiser lake kulifuata basi hilo kwenye njia yake.
Ajali hiyo imetokea wakati polisi jijini humu ikiendesha msako mkali wa magari yenye makosa mbalimbali, katika jitihada zake za kupunguza ajali.
Katika zoezi hilo, zaidi ya magari 40 yamekamatwa.