Na Lilian Lugakingira, Bukoba
JESHI la polisi mkoani Kagera limefanikiwa kukamata bunduki 15, risasi 11 na radio ya upepo moja katika msako mkali unaoendelea katika maeneo mbalimbali mkoani hapa.
Kamanda wa polisi mkoani hapa, Venance Tossi alisema vitu hivyo vilikamatwa katika msako maalum ulioanza Desemba 24 mwaka jana hadi Januari 2, mwaka huu kwa lengo la kuwawezesha wananchi kusherehekea siku kuu kwa amani.
Kamanda Tossi alitaja moja ya mapori yaliyofanyiwa kazi katika kipindi hicho kuwa ni pori la Mitara wilayani Biharamulo ambapo katika pori hilo waliweza kugundua makazi ya majambazi na kufanikiwa kupata vitu mbali mbali zikiwemo bunduki.
Alitaja bunduki zilizokamatwa katika msako huo kuwa ni SMG mbili zenye namba 80 IC 0196 na AP 3183-1989 zikiwa na risasi 11 ambapo risasi mbili zinatumika katika bunduki aina ya SAR na tisa katika bunduki aina ya SMG.
Bunduki nyingine zilizokamatwa ni gobore moja, bunduki zilizotengenezwa kienyeji 12 ambazo zinatumika risasi za SMG/SAR, simu ya upepo, baiskeli tatu, pombe ya moshi lita 20, sanduku na nguo mbali mbali.
Alisema simu ya upepo iliyokamatwa inasadikika majambazi hayo yamekuwa yakiitumika katika mawasiliano na kusikiliza polisi wanapanga nini na wakati mwingine wamekuwa wakijua mapema kuwa itafanyika oparesheni na kukimbia kutoka porini.
Alisema simu hiyo ilikutwa imehifadhiwa katika sanduku hilo ikiwa pamoja na risasi hizo 11, radio ya kawaida, bunduki moja na kisu.
Katika oparesheni hiyo watu sita wanaosadikiwa kuwa ni majambazi walitiwa mbaroni akiwamp mfanyabiashara ambaye aliwahi kukamatwa na bunduki mbili za SMG mwaka 2004.