Kitaifa
   Siasa
   Jamii
   Uchumi
   Makala

 

Search


Advanced Search

 »  Home  »  Mzee Mwanakijiji  »  Mazingaombwe ya RDC na Tanesco!
Mazingaombwe ya RDC na Tanesco!
By Mzee Mwanakijiji | Published  12/29/2006 | Mzee Mwanakijiji | Rating:
Mazingaombwe ya RDC na Tanesco

Kwenye fani ya mazingaombwe kuna vitu vikubwa vitatu. Cha kwanza kinaitwa wepesi wa mikono (sleight of hand), cha pili ni viinimacho (illusion) na cha tatu ni kupoteza lengo (distraction). Ili mazingaombwe yafanikiwe na kuwa na mvuto ni lazima vitu hivyo vitatu viende sambamba na kwa wakati muafaka. Sasa mwanamazingaombwe  aliyebobea atahakikisha kuwa watu wanashuhudia mtu anaingizwa kwenye sanduku (sleight of hand), sanduku linakatwa nusu kwa upanga (illusion) huku mwanamazingaombwe anawaeleza na kuwachangamsha watu kwa maneno na porojo (distraction).

Pindi lile sanduku likiunganishwa tena na yule mtu aliyewekwa humo akatoka mzima (restoration)  basi watu watapiga makofi na kumsifia mwanamazingaombwe wetu kwa onesho zuri na mwanamazingaombwe huyo atachukua pesa zake na kuandaa onesho jingine, na wale ambao hawataki kufikiri juu ya nini wameshuhudia wataendelea kupiga makofi na kuchekelea!

Utamu wa mazingaombwe huharibika pale ambapo watu wanagundua ujanja wa mwanamazingaombwe. Watu wa RDC wameleta mazingaombwe ya hali ya juu na nusura wafanikiwe kumrejesha mtu akiwa bado mzima toka kwenye sanduku. Watanzania walitaka kuridhishwa na onesho zuri la "Umeme". Ndipo wanamazingaombwe toka Houston walipotokea na vikolokolo vyao vya mazingaombwe. Wakawaambia watanzania kuwa wana uwezo wa kuleta nishati (kumkata mtu nusu bila kumuumiza) tena kwa bei rahisi. Watanzania wakaamini na wakawapa nafasi.

Kwa vile wanamazingaombwe wetu hawakuwa na lengo wala uwezo huo iliwabidi wafanye viinimacho. Ndipo wakaagiza "majenereta" ambayo hayakuweza kufika kwa muda muafaka. Wakaanza kuyatengeneza, na kuyaseti ili baadaye yazalishe umeme (ndio kumweka mtu kwenye sanduku kwa taratibu huku watu wakiangalia). Wakaleta na wapiga picha Airport kuona majenereta yanavyoletwa na ndege kubwa zaidi duniani ya mizigo! Watanzania wakapiga makofi na kushangilia!

Wakati watu wanajiuliza hivi kweli wataleta umeme hawa (je kweli mtu ataungika?) basi wanamazingaombwe wa RDC wakaanza kutuhamasisha pamoja na wasaidizi wao (Tanesco) wakilumbana na kukandiana hadharani (distraction). Lengo likiwa kununua muda. Wakati watazamaji (watanzania) wakiendelea kushangaa nini kinaendelea, tukatangaziwa kuwa jenereta  liko tayari kuanza kazi wanasubiri Tanesco wakubali umeme wao. Wakati huo wote, RDC walikuwa wanasubiri mvua!!

Hatimaye, dua zao zikasikika na mazingaombwe ya mwaka yakafanyika. Mabwawa ya umeme yakajaa maji, umeme wa RDC haukutumika, Mkataba wa RDC na Tanesco ukauzwa kwa Waarabu, mwenye kutengeneza pesa akatengeneza pesa, na watanzania wakabakia kushangilia umeme wa kudumu (mgao umeisha)! na Rais Kikwete akashangilia na kuwapongeza viongozi wenzake majasiri, hodari na makini kwa jinsi walivyoshughulikia tatizo la umeme!

Onesho la mazingaombwe la RDC likafanyika kwa ufundi mkubwa. Kwa vile Watanzania hawajagundua kuwa wameshuhudia mazingaombwe, basi mwaka unaokuja watasubiri onesho jingine lenye kuhusu mkataba mwingine, na gurudumu la mazingaombwe na viinimacho linaendelea kubingirishwa!


How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent
Add comment
Comments
  • Comment #1 (Posted by Steve)
    Rating
    Very well put.I hope it doesnt reach a stage where the take the pants off you and you are left clapping.
     
  • Comment #2 (Posted by washawasha)
    Rating
    Aisee poleni sana watanzania wenzangu na mitihani hiyo,ila tuendeleeni kukaza buti safari bado ndefu na tuendelee kustahamili japo tunaumia
     
  • Comment #3 (Posted by Edison)
    Rating

    Mimi naona serikali ya CCM imeshabweteka kuwa chochote itakachofanya, chaguzi zote 2010, 2015, 2020, ... wana hakika watakuwa wanashinda chaguzi.
    Haiwezekani wizara moja ya nishati na madini itufanyie vituko namna hii tangu miaka ya 90.
    IPTL, mikataba feki ya madini na RDC ni mifano ya jinsi watanzania tunavyochukuliwa 'for granted'.

    Maoni yangu ni nini kifanyike: Dawa ni moja tu, kuinyima CCM kura mwaka 2010 ili wajifunze jinsi ya kuwaheshimu watanzania. Hatuwezi kuwachagua miaka yote hiyo halafu wanatufanya majuha!
    Nimesoma jana kuwa Tanesco itakuwa inailipa IPTL sh. bilioni 6.5/= hata kama Tanesco hawatumii umeme wao, Songas nao watalipwa. Sasa kuna unafuu gani kwa Taifa, hata kama mabwawa yamejaa pomoni?
     
  • Comment #4 (Posted by Ndomondo)
    Rating
    Lakini katika mazingaombwe haya kuna tofauti kubwa sana kati ya
     
  • Comment #5 (Posted by Loota L aiser)
    Rating
    Kwa aibu na kubuya sina hata la kusema kwani singaumbwe hili limetupata kweli. Wajinga waliwao.
     
  • Comment #6 (Posted by nagar jalal)
    Rating
    ukweli mtupu sina haja ya kuharibu maudhui ya hoja hiyo,hongera mwanakijiji.
     
Submit Comment


Article Options
Popular Articles
  1. Unaifahamu Jambo Forums?
  2. Ghorofa Jijini lanusurika kuungua moto
  3. Is Tanzania a safe place to invest?
  4. Britsh M.P. calls for the suspension of aid to Tanzania.
  5. Nitaendelea kugombea nafasi za kisiasa- Balozi Karume
No popular articles found.
Popular Authors
  1. Habari Tanzania
  2. Mzee Mwanakijiji
  3. Linda Garner
  4. Nthelezi Nesaa
  5. Marshy Abdu
  6. Prosper Kwigize
  7. Salehe Mmoro
  8. Ramadhan Semtawa
  9. Manyerere Jackton
  10. Ndesanjo Macha
No popular authors found.