BALOZI wa Tanzania nchini Msumbiji, Issa Muhammed Issa, amefariki dunia.
Balozi huyo amefariki dunia jana katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).
Kutokana na kifo hicho, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha balozi huyo.
Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Zanzibar, Nasma Haji Chum, ilisema kuwa marehemu ambaye ametumikia nyadhifa mbali mbali katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Miongoni mwa nyadhifa alizowahi kushika ni pamoja na kuwa Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji kuanzia mwaka 2000 hadi kufariki dunia kwake.
Pia amewahi kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Vijana wa SMZ kuanzia mwaka 1995 hadi 2000, Waziri wa nchi Wizara ya Maji, Ujenzi, Nishati, Ardhi na Mazingira Zanzibar mwaka 1993 hadi 1995.
Aidha aliwahi kushika wadhifa wa Naibu Katibu Mkuu Jumuiya ya Wazazi Tanzania kwa kipindi cha miaka kumi kuanzia mwaka 1983.
Mwaka 1981 hadi 1983 alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Nchi Afisi ya Rais Zanzibar.
Mwaka 1979 hadi 1981 marehemu alishika wadhifa wa Mkurugenzi Mtendaji katika Shirika la Magari Zanzibar, Katibu Mkuu Wizara ya Mawasiliano Zanzibar mwaka 1975 hadi 1977.
Marehemu amewahi pia kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Biashara Zanzibar mwaka 1977 hadi 1979, vile vile alishika wadhifa wa Katibu Mkuu Wizara ya Habari na Utalii 1974, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari na Utalii Zanzibar mwaka 1973 hadi 1974.
Mwaka 1970 hadi 1971 alishika wadhifa wa Naibu Mkurugenzi Mtendaji Utalii Zanzibar na kuwa Mkurugenzi Mtendaji katika kipindi cha miaka mitatu baadaye.
Balozi Issa aliwahi kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi katika vipindi vitatu tofauti hadi mwaka 2000 alipoteuliwa kushika wadhifa wa Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, marehemu amewahi kuwa mjumbe wa bodi ya wakurugenzi katika wizara na idara mbali mbali za serikali, zikiwamo Wizara ya Elimu Zanzibar, katika Idara ya Elimu ya Juu Zanzibar, Hoteli ya Bwawani na TANESCO.
Idara ya Maendeleo ya Wafugaji, Zanzibar, Chuo cha siasa Mbeya, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Tanzania na Shirika la Bima Zanzibar.
Marehemu alizaliwa mwaka 1944 katika Kijiji cha Kiembesamaki Zanzibar na alipata shahada ya kwanza ya Uchumi mwaka 1969 nchini Urusi na diploma ya uongozi katika masuala ya biashara ya utalii nchini Uholanzi mwaka 1971.
“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaungana na familia ya marehemu kuomboleza kifo cha marehemu Balozi Issa Muhammed katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo. Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi. AMIN,” taarifa hiyo ilieleza.