SERIKALI imesema ipo haja ya kutoa elimu zaidi kuanzia shuleni, kuwahimiza wananchi kutambua umuhimu wa kutumia bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi ili kukuza soko lake.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Juma Ngasongwa, alipokuwa akifunga tamasha la kwanza la Uhuru, lililokuwa likifanyika katika viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam.
Ngasongwa alisema kuendelea kuzipa bidhaa hizo kisogo, kutaendelea pia kuwakandamiza wajasiriamali na kuwapunguzia uwezo wa uzalishaji wa bidhaa hizo.
“Katika kipindi hiki cha utandawazi ni lazima tuanze kuzijatiti kwa kuimarisha na kuendeleza soko la ndani ya nchi yetu, na hiyo ndiyo itakuwa nguvu yetu kwa soko la nje,” alisema.
Hata hivyo aliongeza kuwa pawepo na juhudi za makusudi za kuzalisha bidhaa bora ambazo viwango na vifungashio vyake pamoja na bei zake vinakubaliwa katika nchi za jirani.
Ngasongwa aliitaka Halmashauri ya Biashara ya Nje (BET), kuwa na mikakati endelevu ya kutafuta masoko ya bidhaa za ndani, katika masoko ya nchi za jirani kabla ya yale ya mbali.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa BET, Ramadhani Khalfan, aliwahakikishia wajasiriamali walioshiriki katika tamasha hilo kama waanzalishi, kuwa watawaingiza katika mtandao wao na kufanya nao kazi kwa karibu.
Tamasha hilo liliwashirikisha washiriki 246, wakiwamo wajasiriamali wadogo na wale wa kati kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani.