MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi, Taifa, Abiud Maregesi amepinga kampeni zinazoendeshwa na Mbunge wa Jimbo la Rombo, Basil Mramba (CCM) za kutaka kuipokonya jumuiya hiyo umiliki wa Shule ya Sekondari Shauritanga.
Maragesi alitangaza msimamo huo mwishoni mwa wiki wakati wa kikao chake na wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya jumuiya hiyo wa Mkoa wa Kilimanjaro na wale wa Wilaya ya Rombo.
Alisema, shule hiyo haiwezi kuchukuliwa na serikali bila taratibu kufuatwa na kuongeza kuwa, jumuiya ya wazazi kama meneja wa shule, inazo taratibu zake.
Msimamo huo wa Maregesi umekuja wakati kukiwa na kampeni za wazi zinazoongozwa na Mramba, ambaye pia ni Waziri wa Viwanda na Biashara, akishirikiana na wananchi wa Tarafa ya Mashati, za kutaka shule hiyo ichukuliwe na serikali.
Mramba aliwahi kuishambulia jumuiya hiyo akidai kuwa, haina uwezo wa kuiendesha shule hiyo, baada ya matukio mawili ya moto, yalipoikumba shule hiyo mwaka 1994 na kusababisha vifo vya wanafunzi 42 na baadaye tena mwaka 2003 katika tukio ambalo hakuna maafa yaliyotokea.
Wananchi wanaoungwa mkono na Mramba, wamekuwa wakisema kwamba, watoto wao wanaofaulu na kushindwa kuchaguliwa katika shule za sekondari, wanapaswa kuwa na shule karibu, kwani hivi sasa wanashindwa kuwapeleka Shauritanga kwa sababu ya ukubwa wa ada.
Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kwamba, hivi sasa shule hiyo ina wanafunzi wapatao 300 wanaotoka katika tarafa ya Mashati, kata za Katangara Mrere na Mrao Keryo kati ya jumla ya wanafunzi 441 wanaosoma hapo.
Katika kikao hicho, Maregesi aliyekuwa amefuatana na Katibu Mkuu wa jumuiya hiyo, Cosmas Hinju alisema kuwa, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka jana, inaelekeza kuwa kila kata inahitaji kuwa na shule ifikapo mwakani, na kuwataka wanaoinyemelea Shauritanga, waondoe mawazo hayo.
Mwenyekiti huyo ambaye alionekana kukerwa na vurugu zinazoendelea katika shule hiyo, alihoji ni kwa kigezo kipi shule hiyo iwe ya serikali, na kuongeza kuwa, shule hiyo ni mali ya CCM na si vinginevyo.
“Hatuwezi kuitoa shule yetu hivi hivi, tunazo taratibu zetu, na hizi lazima zifuatwe. Hatuwezi kubabaishwa na watu wachache, wala hatumwogopi mtu yeyote,” alisema Maregesi kwa ukali.
Katibu wa jumuiya hiyo wilayani hapo, Hatibu Mnuwa, alisema kuwa, limeibuka kundi la wananchi waishio karibu na shule hiyo, wanaoendesha vitendo vya kihuni katika eneo la shule.
Mnuwa alisema kuwa, kundi hilo limekuwa likivamia shule hiyo, kufanya fujo na kufanya uharibifu mkubwa wa mali za shule, likiwamo eneo ambalo limekusudiwa kujengwa bweni la wavulana.
Aliutaja uharibifu unaofanywa shuleni hapo na wananchi hao kuwa, ni kukata uzio wa shule, kuchukua mawe yaliyonunuliwa kwa matayarisho ya ujenzi na kukata miti katika eneo hilo.