BARAZA la Habari Tanzania (MCT), limeipinga kauli ya Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Muhammed Seif Khatib, kuwa serikali itawasilisha rasimu ya muswada wa uhuru wa habari kama ulivyo, katika kikao cha Bunge, mwezi Aprili, mwakani.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam, jana, Mwenyekiti wa MCT, Profesa Issa Shivji, alisema, wadau wa habari kupitia baraza hilo, wameshangazwa na kauli hiyo na hawakutegemea ingetolewa na waziri anayetumikia Serikali ya Kikwete.
“Kwa umoja wetu, tumesikitishwa na kushangazwa na kauli ya waziri huyu... inaonyesha jinsi anavyolazimisha muswada huo upelekwe bungeni, kisha utungiwe sheria.
“Tunaiomba serikali kuongeza muda kwa wadau kujadili kwa kina rasimu ya muswada huo, na kutoa maoni yao kwa nia ya kuuboresha… ni haki ya kikatiba ya kila mwananchi kupata habari.
“Tunasisitiza… si kweli kuwa rasimu ya muswada huo ilikataliwa na wamiliki wa vyombo vya habari, isipokuwa kwa kauli moja tulikubaliana kwamba muswada haukuzingatia maslahi ya taifa,” alisema Profesa Shivji.
Akieleza sababu za kuikataa rasimu ya muswada huo utakaobana uhuru wa habari, Mwenyekiti huyo wa MCT alisema rasimu hiyo, ina vikwazo vingi vitakavyofanya habari zisipatikane kabisa, na kuifananisha na sheria zilizokuwepo enzi za ukoloni.
Rasimu hiyo, inatoa mamlaka makubwa ya kisheria kwa waziri kuzuia habari kutoka kwenye vyombo vya habari, kudumaza maendeleo ya Watanzania na kuliua kabisa Baraza la Habari nchini.
“Taarifa zozote za serikali zikiwa wazi ni rahisi kupata habari, kupambana na ufisadi na wananchi kutambua mwelekeo na matumizi ya fedha za serikali, lakini rasimu hii itakandamiza haki ya kikatiba ya raia kupata habari.
“Haki ya msingi ya kikatiba ya raia kutoa maoni, kupokea na kutoa habari itakandamizwa, iwapo rasimu ya muswada huo itapitishwa… pia taarifa nyeti za serikali hazitapatikana, kwa sababu ya maslahi ya viongozi wachache, hivyo suala la ufisadi halitakwisha,” alisema.
Shivji, aliiomba serikali kutumia busara na kuwaruhusu wadau wa habari, kuijadili kwa kina na kuifanyia maboresho rasimu ya muswada huo, kabla ya kupelekwa bhungeni na kuwa sheria kamili kwa maslahi ya taifa