HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imetangaza rasmi kuendeleza mazungumzo na Chama cha Wananchi (CUF), mjini Zanzibar kwa lengo la kuleta utulivu na maelewano ya watu katika visiwa vya Unguja na Pemba.
Pia Halmashauri hiyo imemuagiza Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusufu Makamba, kwenda visiwani humo kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wa CCM na vyama vingine vya siasa.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Makamba alisema, NEC ya CCM imetoa uamuzi huo katika vikao vyake vilivyomalizika juzi chini ya mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete ambaye aliahidi mwanzoni kabisa mwa utawala wake kwamba, atalishughulikia tatizo la mpasuko wa kisiasa Zanzibar.
Alisema ameagizwa kufanya mawasiliano na vyama vya siasa visiwani, juu ya umoja kati ya watu wa Pemba na Unguja, ambao sasa hawaelewani kutokana na sababu za kisiasa, ambazo zinawagawa katika makundi makubwa mawili ya vyama vya CCM (Unguja) na CUF (Pemba).
Alisema CCM inatambua manufaa ya kuimarisha mahusiano na vyama vingine vya siasa visiwani na kwingineko nchini, na ndio maana imeamua kuendeleza mazungumzo na vyama hivyo kwa madhumuni ya kudumisha amani, utulivu na maelewano ya watu wa Pemba na Unguja.
Makamba alisema, NEC imeamua kukiimarisha chama chake Unguja na Pemba kiuongozi na kiutendaji na hivyo, inakusudia kuyafanya maeneo hayo kuwa na mradi maalumu katika mradi wa kukiimarisha chama ambao umezinduliwa hivi karibuni.
Katika kukiimarisha chama hicho tawala, Makamba alisema, NEC ya CCM imewateua na kuwahamisha baadhi ya makatibu wa mikoa na wilaya na kupelekwa Pemba na Unguja, mahususi kwa ajili ya programu hiyo.
Aliwataja walioteuliwa kuwa ni pamoja na aliyekuwa Katibu wa CCM Wilaya ya Tanga, Albert Mgumba, ambaye anakuwa Katibu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba; aliyekuwa Katibu wa CCM Wilaya ya Kahama, Adam Ngalawa (Katibu wa CCM Mkoa Kusini Pemba) na Said Shaawe Khamis ameteuliwa kuwa Katibu wa CCM Mkoa wa Kigoma.
Wengine waliohamishwa ni pamoja na aliyekuwa Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Matson Chizii, ambaye amehamishiwa makao makuu ya chama Idara ya Uchaguzi. Aliyekuwa Katibu wa CCM Mkoa wa Shinyanga, John Barongo ameziba nafasi ya Chizii.