WAKAZI wa Kata ya Somangira wilayani Temeke, Dar es Salaam, wamemlalamikia Mkuu wa Wilaya (DC), Abdallah Kihato, kwa kushindwa kufanya mkutano wa hadhara na kusikiliza kero zao.
Wakazi hao wameiambia Tanzania Daima kwamba, viongozi wao walikuwa wamewatangazia kuwa, Kihato angefika kwenye kata yao kujitambulisha na kufanya mkutano wa hadhara.
“Walipita mitaani wakituambia siku hiyo tujitokeze, mwenye kero amweleze DC mpya, tena tufike mapema saa tano, na kweli wananchi tukaacha kazi zetu, tukajitokeza siku hiyo, hata hivyo mkuu huyo alikuja saa saba mchana,” alisema mzee Mpema, mkazi wa Somangira.
Alidai kuwa, baada ya mkuu huyo kufika, viongozi wa kata walimpokea na kwenda kukaa naye kwenye ofisi zao hadi jioni.
Mzee Mpema, alisema wananchi waliendelea kuvuta subira wakidhani kuwa mazungumzo yao yatamalizika mapema ili awahutubie kwenye mkutano wa hadhara bila mafanikio.
Alisema bila shaka viongozi hao walifanya hivyo makusudi ili DC huyo asipate nafasi ya kuzungumza na wananchi kujua maovu yao.
Alipoulizwa na Tanzania Daima kwa njia ya simu, kuhusu kero hizo, DC huyo alisema wananchi hao wanalaumu, lakini hawakujua ratiba yake.
“Ziara yangu ilikuwa ni ya kuongea na maofisa maendeleo wa kata zote, sio kusikiliza kero za wananchi, ipo siku nitafanya hivyo, kule ni eneo langu l