Na Jamal Zuberi, MAELEZO- Dodoma
RAIS Jakaya Kikwete amewapongeza wananchi wa mkoa wa Dodoma kwa kuchangia nguvu zao kwenye ujenzi wa shule mpya 50 za sekondari.
Rais Kikwete alitoa pongezi hizo juzi usiku, kwenye sherehe fupi ya kuhitimisha michango ya elimu, kuchangia ujenzi wa shule za sekondari mkoani Dodoma, iliyofanyika kwenye ukumbi ulioko viwanja vya Bunge.
Mkoa wa Dodoma umekusanya fedha taslimu sh. 638,511,728 kutoka kwa wananchi wa mkoa huo, ambapo kima cha chini cha mchango kilikuwa sh. 5,000.
“Nimehamasika kwa utaratibu huu wa kuchangia kwa lengo la kuendeleza watoto kupata elimu, hii imethibitisha kuwa inawezekana kabisa watu kujitafutia maendeleo wenyewe, bila msaada… inawezekana popote nchini,” alisema Rais Kikwete.
Alikumbusha kuwa ni jambo la aibu kwa binadamu kuombaomba kila wakati au kumsubiri mfadhili katika jambo ambalo linawezekana dhahiri kujisaidia wenyewe.
“Kuchangia sh. 5,000 ni sawa na kuku wawili na inawezekana lakini bila ya moyo wa kuchangia siku zote utatangaza umasikini wako,” alisema.
Alisema serikali itahakikisha kuwa shule hizo mpya zitakaguliwa na kusajiliwa hivyo kupokea wanafunzi wote wa sekondari tayari kwa masomo kuanzia Januari, mwakani.
Awali akitoa maelezo ya michango hiyo ya elimu, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, William Lukuvi alisema wanafunzi 24,078 kati ya 28,679 wamefaulu mtihani wa darasa la
Saba (asilimia 83.95) ya watahiniwa woteikilinganishwa na asilimia 77.79 mwaka jana.
Alisema mkoa umeweza kuchagua wanafunzi 11,315 (asilimia 47) tu ya waliofaulu kwa kutumia shule za zamani, wakati waliobaki 12,763 (asilimia 53) watachaguliwa katika shule mpya ambazo wanaziombea usajili mwezi huu, na nyingine Machi, mwakani.