Na Tiganya Vincent, MAELEZO- Tanga
SHIRIKISHO la Vyama Huru vya Wafanyakazi (TUCTA) mkoani hapa, limekataa wafanyakazi wa wilaya ya Tanga, kukatwa asilimia 10 ya mishahara yao kuchangia kinachodaiwa miradi ya halmashauri ya jiji la Tanga.
Kauli ya kukataa makato hayo ilitolewa jana na Mratibu wa TUCTA mkoa, Innocent Allute, wakati akimkabidhi Kaimu Mkurugenzi wa Jiji hilo, Fortunatus Fwema msimamo huo wa shirikisho hilo.
Mratibu huyo alimweleza Kaimu Mkurugenzi huyo kwamba kikao cha TUCTA cha Desemba 15, mwaka huu kilitafakari kwa kina suala la makato ya asilimia 10 ya mshahara wa mfayakazi kwa maelezo ya kuchangia elimu.
Alisema viongozi wa vyama vya wafanyakazi
wanaujua umuhimu wa elimu na wanakiri kwamba wilaya ipo nyuma katika maendeleo ya sekta hiyo, lakini wanatofautiana na halmashauri ya jiji kuamua kuwakata kiwango hicho watumishi bila ya
kuwashirikisha na kuwahamasisha kushiriki katika mpango huo.
Allute ambaye pia ni Katibu wa TUICO mkoani hapa, alisema TUCTA haikubaliani na suala la kuwakata mishahara wafanyakazi bila ya ridhaa yao na wanaitaka halmashauri hiyo iwaite watumishi wote na kuwahamasisha wakubali kuchangia kwa hiari yao na si vinginevyo.
Alisema siyo utaratibu wa sheria za kazi, mwajiri kukata mshahara wa mfanyakazi bila ya makubaliano na mfanyakazi mwenyewe.
Akizungumza baada ya kikao hicho, Fwema alisema michango hiyo ni kwa ajili ya kufidia ujenzi wa vyumba 44 vya madarasa ambavyo vitagharimu sh. milioni 400.
Fwema alikiri kupokea barua inayoonyesha tamko la TUCTA ikipinga mpango unaotumiwa na halmashauri
kuwakata asilimia 10 ya mishahara yao watumishi wote wilayani humo.
Alisema wameandaa utaratibu wa kukutana na wafanyakazi kuwaeleza nia na madhumuni ya uamuzi huo ambao umelenga kukabiliana na upungufu wa madarasa, ili kuweza kuwapatia nafasi za kuendelea na masomo wanafunzi waliokosa nafasi ya kujiunga na kidato cha kwanza mwakani.