Rais Jakaya Kikwete, ametoa siku saba kuanzia jana kwa uongozi wa soko la kimataifa la mahindi la Kibaigwa kurekebisha tabia ya kuanika mahindi katika mazingira machafu.
Rais Kikwete alitoa agizo hilo jana baada ya kutembelea soko la kimataifa la Kibaigwa na kujionea jinsi mahindi yalivyoanikwa katika mazingira machafu huku wananchi wakiyakanyaga.
Akiwahutubia wananchi katika soko hilo, Rais Kikwete alisema amesikitishwa kuona chakula kinacholiwa na binadamu kinaanikwa katika hali ya uchafu namna ile.
’’Kwa kweli nimesikitishwa na kitendo cha uongozi wa soko kuanika mahindi katika mazingira machafu namna hii, chakula wanachokula binadamu hakiwezi kuanikwa namna hii’’ alisema.
Aliongeza ’’mnayaanika kwenye uchafu, mnaweka kwenye magunia na mnakwenda kuwauzia wananchi, hii tabia yenu mbaya,’’ alisisitiza.
Alitaka apewe taarifa za kujirekebisha tabia hiyo katika kipindi cha wiki moja na kumwagiza Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bw. William Lukuvi, kufuatilia agizo hilo mara moja.
Na katika hatua nyingine, Rais Kikwete aliwaasa wakazi wa Kibaigwa na Chalinze kutunza vizuri chakula watakachovuna katika msimu huu ili kuhakikisha kuwa hawapati tena tatizo la njaa.
Hata hivyo, aliwakumbusha wananchi hao kuwa, mwanzo na mwisho wa msimu wa kilimo ndiyo mwanzo wa maandalizi ya msimu ujao ambapo aliwataka watilie maanani katika kilimo cha mtama na uwele.
Alisema serikali itajitahidi kutafuta mbegu za mtama na uwele wa kutosha kwa ajili ya kusambaza kwa wananchi lakini akawaonya kuwa hawatapewa mbegu za mahindi bali watakaotaka kulima mahindi watafute mbegu wenyewe.
Ziara ya Rais Kikwete pamoja na mambo mengine, ilikuwa na lengo la kuwashukuru wananchi kwa kumchagua katika wadhifa huo na CCM kuongoza dola katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana.