Na Mwandishi Wetu
SAKATA la ununuzi wa korosho katika mikoa ya Kusini limechukua sura mpya baada ya kubainika kuwepo njama zinazofanywa na baadhi ya maofisa ushirika, kuwashawishi wanunuzi kugoma.
Kwa mujibu wa habari za uhakika ambazo gazeti hili limezipata, baadhi ya maofisa ushirika wamepanga njama za kuwashawishi wanunuzi kugoma kununua kurosho kutokana na kuenguliwa katika mchakato wa ununuzi safari hii.
Imebainika kuwa, maofisa hao wameenguliwa kwenye baadhi ya halmashauri, hatua ambayo wameikasirikia na kuamua kushawishi wanunuzi wasinunue korosho au kuzinunua kwa kusuasua.
Kwa mujibu wa habari hizo kutoka maeneo mbalimbali ya mikoa ya Kusini, maofisa hao wanataka korosho zisinunuliwe ili kuwakomoa maofisa wa halmashauri hasa wakurugenzi.
Kutokana na wanunuzi kugoma kununua, wakulima wa korosho katika maeneo ya kusini wamekuwa wakihangaika kupata soko, na wengi kubaki na korosho majumbani mwao.
Hali hiyo imebainika wakati siku alizotoa Rais Jakaya Kikwete kwa wanunuzi wa korosho kununua zao hilo kwa wakulima ulimalizika Jumatatu ya wiki iliyopita, huku wananchi wa eneo hilo wakiona agizo hilo limepuuzwa.
Licha ya agizo hilo, habari zilisema baadhi ya wanunuzi kupitia kwa mawakala wao wamekuwa wakishawishiwa na maofisa ushirika, kuacha kununua korosho ili kushinikiza kubadilishwa kwa utaratibu unaotumika sasa ambao umewaengua katika ununuzi kama ilivyozoeleka.
"Wanataka warudishiwe kazi ya kununua korosho maana katika baadhi ya maeneo, wameenguliwa kabisa na kuwekwa maofisa wengine, ikiwa ni sehemu ya halmashauri kuboresha makusanyo ya mapato," alisema ofisa wa halmashauri katika mkoa wa Mtwara ambaye hakutaka jina lake liandikwe.
Aliongeza kuhoji kuwa: "Inakuwaje katika kipindi kama hiki cha matatizo ya masoko ya korosho na ambacho ni muhimu kwa wakulima wa mikoa ya kusini, baadhi ya maofisa ushirika waende likizo?"
Kwa mujibu wa habari kutoka mikoa hiyo, baadhi ya wanunuzi wa korosho wamekuwa wakitumia ujanja wa kununua kiasi kidogo ili waonekana wanafanya ununuzi na wasifutiwe leseni, lakini ukweli ni kwamba wapo kwenye mgomo baridi.
Jumamosi iliyopita, serikali ilitangaza kufuta leseni za ununuzi kwa kampuni saba kwa kukiuka agizo la Rais Kikwete kuhusu ununuzi.
Mbali na hatua hiyo, serikali imezionya kampuni ambazo zinafanya ununuzi wa korosho kwa kiwango kisichoridhisha, ikilinangishwa na miaka iliyopita.
Hatua hiyo ilitangazwa jana na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wassira, ofisini kwake na kuzitaja kampuni zilizofutiwa leseni kuwa ni Fidahussein Co. Ltd, Kapila Enterprises na Ascrop (T) Ltd.
Nyingine kuwa ni Hebri Enterprises, Compass Services, Annar Cashew factory na Senga Enterprises.
Alisema msimu wa 2006/2007 kampuni 27 zilipewa leseni za kununua korosho na hadi kufikia Desemba 2, kampuni 20 ziliitikia wito wa Rais Kikwete na kununua korosho.
Kwa upande wa kampuni ambazo zinanunua korosho kwa kiwango kisichoridhisha, ukilinganisha na miaka iliyopita, serikali inahimiza kununua korosho kwa kasi na wingi, vinginevyo na wao watafutiwa leseni zao.
Karibuni, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Said Sadick, alikaririwa akisema hali ya ununuzi wa korosho katika mkoa wake bado ni ya kusuasua na katika wilaya ya Liwale kati ya tani 5,000 walizonazo wakulima, zimenunuliwa tani 700 tu.
Aliongeza kuwa lengo la mkoa ni kuuza tani 78,000 za korosho ambapo hadi sasa zilizonunuliwa ni tani 45,000.
Kwa upande wake, Mbunge wa Masasi, Raynald Mrope, alisema kuna tatizo katika ununuzi wa korosho ambao unafanyika kwa 'mwendo wa kinyonga' hivyo kuitaka serikali kuingilia kati kasi iongezeke.
Mrope alisema mikoa ya Mtwara na Lindi ina korosho nyingi, lakini kasi ya ununuzi hairidhishi ikilinganishwa na miaka iliyopita.
"Kwa kweli safari hii hali ni ya kushangaza sana. Kasi ya ununuzi wa korosho ni ndogo tofauti na miaka mingine...sijui kuna jambo gani. Kwa jinsi ilivyo ni vyema serikali iingilie kati," alisema mbunge huyo ambaye ni mwenyekiti wa wabunge wa Mtwara.
Suala la ununuzi wa korosho liliingia kwenye mjadala hata katika kikao cha Bunge kilichomalizika mjini Dodoma karibuni, ambapo Waziri Mkuu Edward Lowassa, aliwaagiza wanunuzi kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa ya kununua kilo moja ya korosho kwa sh. 600 kwa korosho daraja la kwanza na sh. 480 kwa daraja la pili.
Hatua hiyo ilitokana na baadhi ya wanunuzi kuanza msimu wa kununua korosho kwa kutaka kununua chini ya kiwango kilichokubaliwa.
Maeneo yenye matatizo ya ununuzi wa korosho kwa sasa ni katika wilaya za Masasi na Mtwara vijijini kwa upande wa mkoa wa Mtwra na Lindi Vijijini, Kilwa na Liwale kwa mkoa wa Lindi, Tunduru na Namtumbo kwa Ruvuma na mkoa wa Pwani.
Korosho ndiyo zao kuu la uchumi kwa wananchi wa mikoa ya kusini na ambalo lina soko kubwa nchi za nje.