Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Bi Mwanaidi Sinare Maajar amewataka watanzania waliopo nchini hapa kuendeleza mapenzi kwa nchi yao bila kujali wapo ughaibuni ili kuweza kuendeleza taifa lao.Balozi Maajar aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na watanzania katika mkutano wa kwanza baina ya watanzania na Ubalozi wa Tanzania nchini hapa.
Balozi Maajar aliwaasa watanzania hao kuachana na fikra potofu kwamba ni serikali au ubalozi unaoweza kuwaletea maendeleo, ‘’kinachofanyika ni kwa serikali kujenga mazingira na wananchi kutumia fursa zinazotolewa, hivyo basi ni vyema mkafuata ule msemo maarufu wa Rais wa zamani wa Marekani aliesema usijiulize nchi yako imekufanyia nini bali ni nini unaweza kuifanyia nchi yako’’ alisema Balozi Maajar katika hotuba yake ambayo mara kwa mara ilikatizwa kwa makofi.
Aidha akizungumzia malengo hasa ya mkutano huo Balozi Maajar alisema anadhani wakati umefika sasa kwa Watanzania nchini Uingereza kuweza kuwa na umoja wao ambao utawawezesha Watanzania waliopo nchini hapa kuwa pamoja na kupata jukwaa la kutoa na kubadilishana mawazo juu ya yanayoendelea nchini Tanzania na namna wanavyoweza kushiriki.
‘’Umoja ambao ningewashauri muuanzishe utawawezesha ninyi kuwa na fursa ya kudhihirisha utaifa wenu hasa kwa wale ambao mmekuwa nchini hapa kwa muda mrefu na hivyo mtaweza kuwaonyesha watoto wenu utanzania wenu na kuwajenga kizalendo tangu wakiwa wadogo’’ alisema Balozi Maajar.
Mkutano huo uliohudhuriwa pia na maofisa wa Ubalozi akiwemo Mkuu wa Utawala, Bi Radhia Msuya, Mwanasheria wa ubalozi huo, Bi Carolyne Katana, Mwambata wa Ulinzi, Brigedia Jenerali Mwanga, Mkuu wa kitengo cha Uhamiaji, Bwana Sylvester Ambokile, Mkuu wa kitengo cha Fedha, David Nginia, Afisa Utawala,Bwana Kiondo, Mwambata wa Masuala ya Habari na Mawasiliano, Bwana Iddrisa Zaharani.
Katika mkutano huo, Balozi alipendekeza kuundwe kamati ya muda ya viongozi wa jumuiya ya watanzania nchini Uingereza ambayo itapewa jukumu la kutengeneza katiba na kuitisha uchaguzi mkuu wa kuanzisha rasmi jumuiya ya watanzania waishio Uingereza.
Kamati iliyoundwa ina wajumbe kumi ambao ni mwanahabari wa siku nyingi, Juma Pinto, Afisa wa Benki ya New York nchini hapa, Norah Sumari, Mwanasheria Antony Huka, Aliekuwa rais wa serikali ya wanafunzi wa chuo cha IFM Tanzania alieko masomoni Bwana Omari Lambi, Bi Rehan Said Olofi kutoka Zanzibar, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake nchini hapa, Bi Mariam Kilumanga, Mtangazaji wa BBC, Saidi Yakubu, Mmoja wa waanzilishi wa taasisi ya zamani ya Watanzania Bi Lucy Shigikile, na Bwana Hassan Hafidh.
