RAIS Jakaya Kikwete amemteua Balozi Liberata Mulamula, kuwa Katibu Mtendaji wa kwanza, kuongoza Sekretarieti ya Ukanda wa Maziwa Makuu.
Taarifa ya Ikulu jana inaeleza kuwa, Mulamula ni mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo na utadumu kwa miaka minne.
Rais Kikwete alisema kuwa Tanzania imepewa nafasi ya kutoa Katibu Mtendaji, na kwa sababu uteuzi huo ni wa haraka, amemteua mwanadiplomasia huyo mwenye uzoefu wa muda mrefu.
Mara baada ya taarifa hiyo, ukumbi mzima ulilipuka kwa shangwe na vigelegele, hali iliyodhihirisha kukubalika kwa uteuzi wa Rais Kikwete.
“Shangwe hii inadhihirisha kukubalika kwa mteule wetu,”alisema Rais Kikwete, hali iliyoamsha shangwe kutoka kwa wajumbe wa mkutano.
Mara baada ya uteuzi huo, Balozi Mulamula aliahidi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa, na kushirikiana kwa karibu na viongozi wakuu wa nchi hizo, ili kuhakikisha kwamba amani, utulivu na maendeleo yanatawala katika eneo hilo.
Kabla ya uteuzi huo, Balozi Mulamula alikuwa Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Katika mkutano huo, Rais Kikwete alisema kuwa Tanzania inaahidi kutoa dola za Marekani 259,366 kusaidia sekretarieti ya ukanda huo na dola 500,000 kwa ajili ya mfuko maalumu wa ustawishaji na maendeleo.
Ofisi za Sekretariati ya Ukanda wa Maziwa Makuu itakuwa Bujumbura, Burundi