MWANAMKE anayedai kuzaa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) mstaafu, Omary Mahita, Rehema Shabani, amemtaka mkuu huyo kuithibitishia mahakama kwamba hakuwahi kuwa na uhusiano naye wa kimapenzi.
Akiwasilisha majibu ya pingamizi lililotolewa na Mahita, jana aliiambia mahakama kuwa hoja za pingamizi la Mahita, hazina ukweli kwani kipindi alichokuwa mtumishi wake wa ndani, walikuwa na uhusiano wa kimapenzi uliosababisha kupata ujauzito wa mtoto wa kiume wa miaka 8.
Mbele ya Hakimu Pellagia Khaday wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Rehema alipinga dai la Mahita, kutotambua kuzaliwa kwa mtoto na kufahamishwa jina la mtoto, akisisitiza kwamba, alikuwa na taarifa za ujauzito hadi kuzaliwa kwa mtoto.
Katika majibu hayo, Rehema, alidai pia kuwa Mahita, aliwahi kumpa fedha za matumizi ya mtoto huyo na baada ya muda, aliacha kutoa, na kwamba hiyo ndiyo sababu ya kumfungulia kesi ya madai.
Aidha, alikanusha pingamizi lililotolewa na Mahita kupitia wakili wake, Charles Semgalawe, kwamba mwaka 2003 alikwenda nyumbani kwa Mahita, Mtaa wa Bogoyo, Oysterbay na kufanya fujo na kueleza kuwa alikwenda kufuata fedha za matumizi ya mtoto.
Alieleza, Mahita alihisi kwamba mkewe (ambaye sasa ni marehemu), angefahamu kuhusu mtoto, akawaamuru askari walinzi wa nyumbani kwake kumpeleka Rehema na mwanawe kusikojulikana kwa ahadi ya kumpa fedha, lakini mmoja wa walinzi hao aitwaye Peter, alimchukua mtoto na kumpeleka kwa Shekh Yahaya.
Baada ya kuwasilisha majibu hayo, Hakimu Khaday, alisema, mahakama itasikiliza pingamizi la kutaka kufutwa kwa kesi hiyo kwa njia ya maandishi, Desemba 30, wakili wa Mahita, atawasilisha maelezo ya kutaka kufutwa kwa kesi.
Hakimu huyo alimtaka mlalamikaji kuwasilisha majibu ya maelezo ya mlalamikiwa Januari 15 mwakani. Kesi iliahirishwa hadi Januari 22 mahakama itakapotoa uamuzi wa ama kuendelea nayo au kuifuta.
Katika kesi hiyo, Rehema, anadai kulipwa fidia ya sh 100,000 kila mwezi kama malipo ya matunzo ya mtoto kuanzia mwaka 1997 hadi atakapomaliza shule.
Rehema, aliwahi kuwa mtumishi wa ndani nyumbani kwa Mahita akiwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro (RPC) mwaka 1996 kipindi ambacho alianza uhusiano wa kimapenzi na Mahita.