WIZARA ya Afya na Ustawi wa Jamii, imeombwa kuwaondelea kielimu watumishi wake mkoani Ruvuma.
Ombi hilo limetolewa na watumishi hao wakati wakizungumza na Mwananchi kuhusiana na vikwazo wanavyokumbana navyo katika utekelezaji wa kazi zao kutokana na kukosa ujuzi wa kutumia vifaa vya kisasa.
Mmoja wa wafanyakazi hao ambaye ni Fundi Msanifu Msaidizi Kitengo cha X-ray na Ultrasound, Moza Chita alisema watumishi wengi wa sekta hiyo wanahitaji kujiendeleza hasa katika kipindi hiki cha matumizi ya teknolojia za kisasa.
Chita alitoa mfano wa vifaa vya kisasa vikiwamo vya maabara ambavyo wamekuwa wakipelekewa kuwa imekuwa ni vigumu kwao kuvitumia kutokana na kuhitaji ujuzi zaidi.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma , Dk Luitfrid Komba ameiomba serikali kuwaendeleza watumishi hao ili waweze kuisaidia jamii kuboresha afya za watanzania.
“Watumishi wengi wanahitaji elimu na wameonyesha nia ya kujiendeleza kimasomo, lakini wanakwamishwa na hali ngumu ya maisha kwani maslahi yao ni duni na haya watoshelezi kuendesha maisha yao,” alisema Dk Komba
Awali, watumishi hao, waliitaka serikali kuiangalia upya sekta hiyo ya afya kwa kuwaongezea maslahi na kuwalipa malipo ya ziada na dharura.