Na Midraji Ibrahim TAASISI ya Kuzuia Rushwa nchini (PCB), imesema rushwa imekithiri katika Idara ya Misitu na Wanyamapori, hivyo imelazimika kuifanyia kazi kwa karibu zaidi.
Akizungumza ofisini kwake katika mahojiano maalum na Mwananchi Jumanne wiki hii, Mkurugenzi Mkuu wa PCB, Edward Hoseah, alisema awali taasisi yake iliipuuza Idara ya Misitu na Wanyamapori, lakini taarifa walizonazo zinaonyesha kuwa idara hiyo imekithiri kwa rushwa.
"Hilo liko wazi, rushwa ipo kubwa kwenye Idara ya Misitu na Wanyamapori, huko nyuma hatukuitazama... sasa hivi vijana wangu wanafanya kazi kwa karibu na idara hizo," alisema Hoseah.
Kumekuwepo malalamiko ya rushwa ndani ya idara hiyo, hali iliyosababisha aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Anthony Diallo, kuwashutumu watumishi wa idara hiyo kwamba kwa sehemu kubwa wanahusika na uvunaji haramu wa miti.
Utaoji wa vibali vya kusafirisha magogo, umekuwa ukitiliwa shaka kutokana na kupuuzwa kwa maagizo ya serikali kupiga marufuku usafirishaji huo, wafanyabiashara wameendelea kusafirisha magogo bila kukamatwa na watumishi wa maliasili.
Idara ya Wanyamapori, imekuwa ikidaiwa kutawaliwa na rushwa ambayo husababisha wawindaji wazalendo kupewa maeneo yasiyo na wanyama, huku wawindaji kutoka nje wakipewa maeneo yenye wanyama na yasiyoruhusiwa kwa shughuli za uwindaji.
Katika ripoti iliyoandikwa na R.D Baldus kutoka Mbuga ya Hifadhi ya Saadani, Bagamoyo na A.E Cauldwell wa Miradi ya Mapori ya Akiba ya Kagera na Kigoma, waliainisha sehemu mbalimbali ambazo zimekuwa zikitiliwa mashaka ya rushwa kwa upande wa wanayamapori.
"Kundi moja la makampuni ambalo liko chini ya mmiliki mmoja, limepewa vitalu 20 vya uwindaji ambavyo ni sawa na asilimia 35 ya vitalu vyote vilivyoko mbuga ya Selous," inasema ripoti hiyo.
Masuala mengine yanayoainishwa kwenye ripoti hiyo kuwa yananuka rushwa ni ukomo wa muda wa vibali vya umiliki wa vitalu. Wakati sheria inataka mmiliki kurejesha eneo baada ya miaka mitano, kuna kundi la makampuni ambayo mmiliki wake ni mmoja, yameshikilia vitalu hivyo tangu mwaka 1978.
Hoseah, alisema baada ya kuandikwa kwenye vyombo vya habari, wamefuatilia na kubaini kuwepo rushwa kubwa na kwamba, hivi sasa wako kwenye mchakato wa kuwanasa wahusika na jinsi ya kukomesha vitendo hivyo