Na Midraji Ibrahim UDANGANYIFU katika mtihani wa darasa la saba uliofanyika Septemba mwaka huu, umeishtua Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na kulazimika kusitisha kutangaza viwango vya ubora na ufaulu wa kila mkoa.
Kutokana na udanganyifu huo uliogundulika wakati wa usahishaji wa mitihani, wanafunzi 294, wakiwamo watatu wasioona, wamefutiwa matokeo baada ya kubainika kuwa walihusika na vitendo vya udanganyifu, huku matokeo ya wanafunzi 2,677 yakishikiliwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Akitangaza matokeo hayo jana, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Margaret Sitta, alisema matokeo ya watahiniwa hao yamesitishwa kutokana na kuwepo kwa dalili za udanganyifu katika mitihani na uchunguzi dhidi yao unaendelea.
Sitta alisema watahiniwa watakaothibitika kushiriki udanganyifu huo watafutiwa matokeo kwa mujibu wa kanuni za mitihani na kwamba ambao hawatathibitika watapewa matokeo yao.
"Matokeo ya ufaulu kwa kulinganisha mikoa hayatatangazwa kutokana na udanganyifu uliojitokeza katika baadhi ya mikoa nchini," alisema Sitta na kuongeza kuwa, mitihani haikuvuja bali kilichofanyika ni udanganyifu mbalimbali. Matokeo ya watahiniwa ambao hawabainika kufanya udanganyifu yatatolewa leo katika mikoa yote.
Waziri huyo, aliwahakikishia wananchi kuwa waliohusika na udanganyifu huo watachukuliwa hatua kali za nidhamu na sheria, huku akisita kutangaza aina ya hatua zitakazochukuliwa.
"Sio rahisi kutoa jibu la hatua gani zitachukuliwa, lazima tujue kwanza aina na kiwango cha udanganyifu...kila mwaka umekuwepo udanganyifu, lakini mwaka huu tumeamua kuwa wazi," alisema.
Kuhusu kiwango cha wanafunzi waliofaulu, Waziri Sitta alisema watahiniwa 664,323 walifanya mtihani huo na kati ya hao, watahiniwa 468,187 sawa na asilimia 70.48 wamefaulu ukilinganisha na kiwango cha kufaulu cha asimilia 61.67 mwaka jana.
Wasichana 211,224 kati ya 327,006 wamefaulu sawa na asilimia 64.6, huku wavulana 256,963 kati ya 337,317 sawa na asilimia 76.2 wakiwa wamefaulu. Jumla ya wanafunzi 686,192 walijiandikisha kufanya mtihani huo, lakini waliofanya mtihani ni 667,294 sawa na asilimia 97.2. Watahiniwa 18,898 hawakufanya mtihani.
Sitta alisema sio chini ya asilimia 70 ya waliofaulu watakaojiunga na sekondari na kuwataka wasichana kuongeza kasi zaidi katika masomo ili waweze kufikia kiwango cha wavulana na hata kuwapita na kutoa ushindani.
Katika hatua nyingine, Waziri Sitta alisema Februari mwakani, serikali inatarajia kuajiri walimu kwa ajili ya kukabiliana na idadi kubwa ya wanafunzi watakaochaguliwa kuingia sekondari.
Alisema ongezeko la kiwango cha kufaulu ni sehemu ya mafanikio ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (Mmem) ambao umeboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, ikiwamo ongezeko la vyumba vya madarasa, vyoo, upatikanaji wa samani, maji, ajira ya walimu, vitabu na vifaa vingine.
Takwimu za Sitta zinaonyesha kuwa kiwango cha kufaulu kimekuwa kinaongezeka mwaka hadi mwaka ambapo mwaka 2002 waliofaulu walikuwa ni asilimia 27.1; mwaka 2003 (40.1%), mwaka 2004 (48.68%) na mwaka 2005 wasilimia 61.76.