KWA mara ya kwanza tangu aingie madarakani takribani mwaka mmoja uliopita, Rais Jakaya Kikwete, jana alifungua Baraza la Biashara la Taifa na kutoa tamko muhimu kuhusu uhusiano utakaoongoza utawala wake na sekta binafsi.
Rais alisema wazi kwamba utawala wake utaendelea kuwa na uhusiano mzuri na sekta binafsi; kuisaidia ili kuona kwamba inakuwa na kuchukua dhima ya kuwa injini ya uchumi wa taifa hili.
Rais pia aliahidi kwamba ni nia ya utawala wake kuona kwamba vikwazo vyote vya kufanya biashara nchini vinaondoka ili shughuli za kibiashara ziweze kushamiri na kuongeza ajira kwa Watanzania ili wawe na maisha ya neema zaidi.
Kwa bahati nzuri zaidi, Rais aliwahakikishia washiriki wa mkutano huo unaofanyika katika Hoteli ya Kilimanjaro Kempinsiki, kwamba anataka kuwa msikilizaji zaidi ili ajifunze zaidi kutoka kwa washiriki wake na ndiyo maana aliotoa hotuba fupi ya ufunguzi na akaomba mkutano huo usiwe ni wa kuzungumza tu bila kufuatiwa na vitendo na majukumu ya dhati.
Tunatambua kwamba Rais anaingia kwenye viatu vya mtangulizi wake, Rais Benjamin Mkapa, ambaye alishiriki katika uanzishwaji wa Baraza hilo, lakini pia akawa mwenyekiti wake. Ni habari njema kwamba Kikwete naye atafuata nyayo za Mkapa katika kufufua nguvu ya sekta binafsi ambayo sababu za kisera huko nyuma chini ya uchumi dola ilikufa.
Tunajua kwamba tangu Tanzania ianze mageuzi ya kiuchumi miaka ya mwisho ya themanini na kuimarika zaidi miaka ya tisini kabla ya kushika kasi miaka ya 2000, sekta binafsi imeweza kugeuza mwelekeo wa uchumi wa nchi hii kwa kiwango kikubwa.
Ajira nyingi siku hizi ziko kwenye sekta binafsi, uzalishaji wa bidhaa na utoaji huduma za aina mbalimbali vinasukumwa na nguvu ya sekta binafsi. Ulipaji kodi kama mapato halali ya serikali na hivyo kuiwezesha kutekeleza majukumu yake muhimu kama ujenzi wa miundombinu na ulinzi na usalama taifa, ni matokeo ya kuimarika kwa sekta binafsi.
Kwa hiyo Rais kuamua kukutana na wafanyabiashara hawa ni jambo la kupigiwa mfano na kwa kweli wengi walikuwa wakihoji kwa nini mkutano huu umechelewe sana kufanyika.
Wanahoji hayo si kwamba ni wazandiki, la hasha, ni wakereketwa wa maendeleo ya taifa hili ambao wangependa kusikia kutoka kwa Rais wao kwamba utawala wake umejipanga je katika kushirikiana na sekta binafsi, ili kujenga makubaliano ya pamoja.
Lakini kubwa zaidi mikutano huo ni muhimu kwa serikali mpya kueleza utashi wake wa kisiasa katika ama kuendeleza yake ya awamu ta tatu au hata kuongeza hatua zaidi ili azma ya kuiwezesha sekta binafsi kuwa injni ya uchumi wa nchi iweze kutimia.
Kwa kutambua maana na nguvu ya mkutano huu, tungependa kumpongeza Rais kwa kukubali kuvaa viatu vya Rais Mkapa katika kuendeleza Baraza hili, lakini pia kwa changamoto aliyoitoa Rais jana, kwamba mkutano huo usiwe ni jukwa la maneno tu.
Rais ametoa changamoto kwamba mkutano huo uwe ni wa kazi, kukaa na kupanga mikakati, kupeana majukumu ili kila mmoja baada ya kumalizika mkutano huo ajue anao wajibu wa kwenda kutekeleleza, kwa nia ya kuijenga Tanzania yenye mafanikio mazuri zaidi kiuchumi.
Ni kwa kufanya hivyo tu, yaani kupeana majukumu, muda wa kuyatekeleza na kupima ufanisi wake, kwa kila mmoja kutambua anayo dhima mbele yake; mkutano huu utakuwa na maana. Tunaamini wakati ndiyo huu wa kujengeana utamaduni wa kuwajibika kila mmoja kwa nafasi yake, serikali sawia na sekta binafsi