Na Mwandishi Wetu UKIRITIMBA wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco) katika kusambaza nishati hiyo nchini unaelekea kufikia kikomo, baada ya kampuni binafsi ya Mtwara & Lindi Energy Project kuruhusiwa kusambaza nishati hiyo katika mikoa hiyo.
Kampuni hiyo inayotarajiwa kuanza kuzalisha megawati 24 za umeme unaotokana na gesi ya Mnazi Bay baada ya wiki moja, itakuwa inasambaza na kuuza umeme wake kwa watumiaji bila kupita kwanza kwa Tanesco.
Habari ambazo Mwananchi imezipata zimesema kuwa Tanesco limeshafungasha virago na wafanyakazi wake waliokuwa katika mikoa ya hiyo wamekwisha kulipwa mafao yao na kuachishwa kazi na kuwa baadhi yao wameajiriwa upya na kampuni ya Artumas inayoendesha kampuni ya Mtwara & Lindi Energy Project.
Hata hivyo, alipoulizwa jana, Meneja Uhusiano wa Tanesco, Daniel Mshana, hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo.
Uzinduzi wa uzalishaji wa umeme kutoka katika gesi hiyo ulifanyika katika kitongoji cha Ruvula, Msimbati, Mnazi Bay, Wilaya ya Mtwara Vijijini Desemba 9, wakati Tanzania inaadhimisha miaka 45 ya Uhuru wake.
Akiwa ziarani mkoani Mtwara hivi karibuni, Rais Jakaya Kikwete, aliitaka kampuni hiyo kutouza umeme wake kwa bei ya juu kuliko Tanesco, kwani serikali imeshaipatia Sh14 bilioni kama ruzuku ili kufidia sehemu ya gharama zake.
Vile vile serikali imetoa Sh22 bilioni zaidi ili kuwekeza katika kusambaza njia ya umeme katika baadhi ya wilaya za mikoa hiyo ili kuhakikisha umeme unafika katika maeneo ya vijijini.
Gesi kwa ajili ya kuzalisha umeme huo ilianza kutiririka katika bomba la kilomita 27.4 linalopita chini ya bahari na nchi kavu hadi Mtwara mwishoni mwa wiki, na inatarajiwa kuzalisha umeme baada ya wiki moja.
Mkurugenzi Mkuu wa Artumas, Peter Gathercole, alisema katika taarifa yake kuwa kampuni yake imeanza majaribio ya umeme huo katika jenereta sita na itaanza kufanya majaribio katika mitambo itakayopokea gesi hiyo, mara baada ya kuunganisha vifaa vyake ambavyo imevipata hivi karibuni kutoka Nairobi, Kenya.
Hata hivyo, vifaa hivyo vimechelewa kuwasili kwa wiki moja, hivyo kusababisha mji wa Mtwara kuchelewa kupata umeme ambao uliahidiwa kuwa ungepatikana Desemba 8 mwaka huu.
Alisema uzinduzi wa mwanzo wa mitambo kwa ajili ya kuunganisha katika mtandao wa usambazaji umeme katika mji wa Mtwara umekwisha kuanza.
"Jenereta sita za kw2000 zinaandaliwa kupokea gesi na kuanza mchakato wa kuwasha mtambo wa umeme. Kazi hii infanywa kwa haraka iwezekanavyo, lakini bila kuhatarisha usalama wa watu na vifaa vyenyewe," alisema.
Alisema Tanesco wataunganisha umeme kati ya vijiji vya Mbuo na Namunda ili kuipatia Lindi umeme kutoka Mtwara.
Akizungumza juu ya kupeleka umeme mkoa wa Lindi, Gathercole alisema kuwa baada ya kukamilisha mazungumzo na serikali, kampuni ya Artumas itazifanyia ukarabati na kuboresha njia za usambazaji umeme katika mkoa huo.
"Mara gesi itakapofika Mtwara na umeme kuzalishwa, viwanda vya mbolea, plastiki na miradi midogo midogo vitatoa ajira na kuboresha maisha ya wakazi wa Mtwara na Lindi. Vile vile, viwanda vya korosho ambavyo havifanyi kazi vitafufuliwa na kuongeza uzalishaji,"ť aliongeza.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Henry Shekifu, aliuambia umati uliokuwa unasherekea miaka 45 ya Uhuru kuwa mradi wa gesi wa Mnazi Bay utahamasisha uwekezaji na kujenga uhusiano wa kiuchumi katika sekta mbalimbali za kijamii.
Shekifu alisema tayari wawekezaji wameanza kuulizia maeneo ya kuwekeza, na kuongeza kuwa mamlaka ya Mkoa imetenga hekta 2,600 za ardhi katika eneo kuzunguka bandari ya Mtwara