MKURUGENZI Mkuu mpya wa Taasisi ya Kuzuia Rushwa nchini (Takuru), Edward Hosea, ameanza kazi kwa kasi mpya baada ya kuamua kutangaza kwenye vyombo vya habari namba zake za simu na zile za watendaji wake.
Kiongozi wa kwanza kufanya hivyo, alikuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali, Said Mwema pindi alipoteuliwa na kuachana na ukiritimba uliokuwa unafanywa na aliyemtengulia, Omari Mahita.
Hatua ya Mwema kutoa namba yake ya simu na zile za wakuu wa polisi wa mikoa, imesaidia kupokea matukio mengi ya uhalifu moja kwa moja kutoka kwa wananchi.
Hosea, baada ya kuapishwa Jumatatu wiki hii, alilielezwa Mwananchi kuwa anakwenda kuanza kazi kwa ari, nguvu na kasi mpya na kwamba atadhihirisha mabadiliko ya utendaji wa Takuru katika miezi sita ijayo.
"Usiniulize kasi mpya sasa hivi. Njoo baada ya miezi sita uniulize kasi mpya niliyowaahidi. Kuapa sio ufumbuzi wa matatizo bali ni mwanzo wa safari," alisema Hosea wakati akijibu maswali ya mwandishi wa Mwananchi.
Namba yake ni 0754 763741, Naibu wake, Lilian Mashaka ni 0754 336116, Mkurugenzi Idara ya Utafiti, Udhibiti na Takwimu ni 0754 336060, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Upelelezi, Alex Mfungo ni 0784 998841 na Kaimu Mkurugenzi Idara ya Elimu kwa Umma, Mary Mosha ni 0784 998836. Namba za wakuu wa Takuru mikoa pia zinapatikana kwenye gazeti la jana.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, kuhusu uamuzi wa kutoa namba zake na wakuu wa Takuru wa mikoa, Hosea alisema katika uongozi ameamua kuwa muwazi na kuomba wananchi kutoa ushirikiano kwa taasisi hiyo.
"Kama hukutangaza simu hizo na kuonyesha uwazi huo, mwananchi wa kawaida sio rahisi kujua namba yangu ya simu na pindi anapopata taarifa za rushwa na kama akikwama sehemu zingine anaweza kuona ndio mwisho, nimeona ni bora tutoe namba za simu ili tuweze kufikika kwa urahisi," alisema Hosea.
Alisema hakuna siri kwenye taasisi hiyo ambazo zinaweza kuwafanya kuficha namba zao za simu na kwamba, iwapo wangeendelea kufanya hivyo wangekuwa wanajikwamisha wenyewe kiuntendaji.
Mkurugenzi huyo, ambaye kabla ya kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete alikuwa Naibu Mkurugenzi wa Takuru, alisema wananchi lazima wafahamu kuwa taasisi hiyo haina ubwana wala utwana, bali waliopo ni watumishi wao.