Na Mwandishi Wetu BENKI ya Watu wa Zanzibar (PBZ) inayomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetangaza kuuza asilimia 60 ya hisa zake kwa wawekezaji watakaojitokeza.
Wizara ya Fedha na Uchumi Zanzibar imetoa taarifa hiyo kupitia vyombo vya habari iliyotiwa saini na Katibu Mkuu wake, Khamis Mussa.
PBZ alianzishwa mwaka 1966 na hadi kufikia Desemba 2005 ilikuwa na mtaji wa Sh60.5 bilioni.
Serikali imesema katika taarifa yake kwamba inakaribisha wawekezaji watakaoongeza mtaji wenye uwezo wa uzoefu huku wakiwa na sera na ari ya ubunifu kwa ajili ya kuendesha benki hiyo.
Lengo kuu la kubinafsisha benki hiyo ni kuleta mabadiliko na ushindani wa kiuchumi Zanzibar kutoka kuwa uchumi wa msingi wa kutumia sana fedha na kuwa uchumi wa msingi wa huduma za kibenki.
Katika mabadiliko hayo ya kuibinafsisha PBZ, muwekezaji anatakiwa kuibadilisha benki hiyo na kuwa yenye kutumia vifaa vya kisasa huku ikiendelea na malengo yake ya kutoa mikopo midogo midogo kwa wananchi.
Taarifa ya benki hiyo imesema kipindi cha mchakato kitafikia ukingoni Machi mwakani ambapo orodha ya wawekezaji waliowasilisha maombi yao itafanyiwa kazi na mshindi kupatikana.
Awali SMZ ilitangaza azma yake hiyo ya kuibinafsisha PBZ katika kikao cha Baraza la Wawakilishi kilichomalizika miezi miwili iliyopita na Waziri wa Fedha na Uchumi, Dk Mwinyihaji Makame.
Wafanyakazi wa Benki hiyo wamekuwa na wasiwawasi mkubwa tangu kutangazwa azma hiyo na hatma yao haijajulikana kwa vile kuna idadi kubwa ya wafanyakazi katika benki hiyo.
Benki Kuu ya Tanzania BoT katika mwaka 1995 iliitaka PBZ kufunga matawi yake mawili ya Wete na Mkoani ya kisiwani Pemba baada ya kubainika kuwa na hali ngumu ya kifedha na kuwepo hatari ya kufilisika. Hivi sasa benki hiyo ina tawi moja tu la Wete kisiwani Pemba.
Kwa upande wa Unguja, yamebaka matawi mawili tu ambayo moja ni Makao Makuu Shangani na jingine liko nje kidogo ya mji wa Zanzibar eneo la Mwanakwerekwe.
Benki hiyo iliyafunga matawi yake yote ya vijijini ikiwemo Mkwajuni, Chwaka na Makunduchi mwaka 1998 ikiwa ni utekelezaji wa agizo la BoT ambayo ndio chombo cha mwisho cha kusimamia masuala ya fedha na ya kibenki nchini.