.Ilikuwa wakati wa kampeni za uchaguzi
.DCI asema tayari upelelezi umekamilika
MKURUGENZI wa Mashitaka (DPP) amepokea jalada la mbunge anayedaiwa kutoa taarifa za uongo kuhusu elimu yake wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka jana.
Akizungumzia suala hilo ofisini kwake, Mkurugenzi wa Mashitaka, Geoffrey Shaidi, alithibitisha ofisi yake kupokea jalada hilo.
“Jalada limefika leo mezani kwangu… limepokewa ofisini Juni 6,” Shaidi alisema jana.
DPP ambaye hakuzungumzia undani wa jalada hilo, alisema ofisi yake italishughulikia na hakutaka kutaja jina la mbunge kwa wakati huu.
Awali, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba, akizungumza na Uhuru alisema ofisi yake imekamilisha upelelezi kuhusu mbunge huyo na kuwasilisha jalada kwa DPP.
Manumba alisema ofisi yake ilipata taarifa za malalamiko kuhusu mbunge huyo na si kweli kwamba inawahoji wengine kadhaa.
Baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti kuwa wabunge kadhaa wamehojiwa na polisi kwa kughushi vyeti vikiwemo vya elimu.
Kutoka gazeti la Uhuru
Na Esther Mvungi