Na Elizabeth Mjatta
BAADA ya kupata dhamana, viongozi watano wa kiwanda cha kutengenezea nguo cha NIDA Textiles wanaokabiliwa na kesi ya kujeruhi na kumfungia ndani mfanyakazi wao,wameomba hakimu Eddy Lyamuaya, kujitoa katika kesi hiyo wakdai hawana imani naye.
Ombi hilo liliwasilishwa mahakamani hapo jana na wakili anayewatetea, Said El Maamry. Wanadai kuwa hakimu huyo anaonekana kutowatendea haki kwa kuwa aliwapa masharti magumu kabla ya kuwapa dhamana.
“Mheshiwa hakimu nakushauri kwa heshima ujitoe kwani wateja wangu hawana imani na wewe tangu kipindi kile cha maombi ya dhamana na pia jinsi ulivyokuwa ukiwauliza maswali wadhamini ulikuwa unawabana sana ili watuhumiwa waendelee kusota rumande bila sababu za msingi” alidai wakili huyo.
Baada ya ombi hilo Mwendesha Mashitaka Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Kanda Maalumu ya Mkoa wa Dar es Salaam, Charles Kenyella, aliomba muda wa saa 24 kwenda kupitia vifungu hivyo vya sheria na leo uamuzi utatolewa.
Jana mlalamikaji katika kesi hiyo Kheri Adinani Khalifa alitakiwa kutoa ushahidi wake ambapo ilishindikana baada ya wakili kutoa pingamizi hilo.
Washtakiwa wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Habib Ghani (30), Muhamad Rashid (25), Shahzad Hassan (36), Iman Jaboon (25) pamoja na Atif Muhammada (30) wote wanaishi ndani ya kiwanda kilichopo maeneo ya Tabata Relini jijini Dar es Salaam.
Washtakiwa hao kwa pamoja walikubali maelezo yote yanayohusiana na vibali vinavyowaruhusu kukaa nchini na kufanya kazi na kukataa kuhusika katika tukio la kujeruhi mfanyakazi huyo na kumfungia ndani ya kontena.
Wanadaiwa kuwa Julai 12 majira ya saa 5:30 asubuhi katika cha NIDA kwa makusudi na kinyume cha sheria walimshambulia kwa kutumia vipande vya nondo na kisha kumfungia ndani ya kontena.