*Awapongeza kwa uzalendo wao kujadili masuala ya kitaifa
*Awaasa kutofanya masikhara na siasa wala viongozi
*Watanzania walio mtandaoni wamjibu, wengine wamwuliza maswali kedekede
Katika hatua ambayo imeonyesha kuwafurahisha watanzania watumiao mtandao wa intanet walio ndani na nje ya Tanzania, Mhe. Freeman A. Mbowe amejitokeza na kujisajili katika Mtandao mmoja na kutoa maoni yake kama watanzania wengine wafanyavyo.
Hali hii imewafurahisha watanzania walio wengi kwani badala ya kuendelea kuongea mambo bila kuwa na mlengwa wa kuelekeza maswali yao na kero zao kwake wamempata kirahisi na kumwuliza au kumpa ushauri wao harakaharaka.
Tarehe 2, Desemba 2006 Mheshimiwa Mbowe alijisajili katika
www.JamboForums.com na kueleza hisia zake & shukrani kwa watanzania ambao wamekuwa wakichangia katika mijadala mbalimbali mtandaoni.
Baadhi ya watanzania waliomhoji au kutoa shukrani zao wamempongeza Mhe. Mbowe kwa kutumia njia ya mtandao na kujiweka bayana. Wengine walionekana kutofurahishwa na kitendo chake kujiweka bayana wakidai kuwa inaweza kumwaribia jina.
Maoni mbalimbali yametolewa na Mhe. Mbowe aliahidi kutoa majibu moja baada ya jingine (hasa yatakayoonekana ya msingi).
Tunapenda kuungana na watanzania wenzetu kumshukuru Mhe. Mbowe kwa kuingia mtandaoni bila kujificha ili watanzania waweze kumwuliza maswali mbalimbali na tunamwomba asiwadharau au kuchukia pale atakapoulizwa maswali yanayoelekea kuwa na dhamira mbaya. Atambue wazi kuwa wanadamu hatufanani na lazima kuna wanaomuunga mkono na wasiomuunga mkono.
Aidha ingependeza viongozi zaidi wa kitaifa wangetumia fursa hii ya mtandao kuweza kuwafikia wananchi mbalimbali kwani wanakuwa wanatoa dukuduku zao bila kificho na bila wasiwasi.
Kupata kujua watanzania wamemwuliza maswali gani na amejibu nini Bofya hapa:
www.JamboForums.com