Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, John Magufuli,amesema kuwa atawafukuza kazi mara moja mameneja wa Shirika la Nyumba nchini (NHC) watakaobanika kuwa wabovu.
Alitoa tishio hilo jana wakati akifungua kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa shirika mjini Morogoro.
’’Nitawafuatilia mameneja wanaolalamikiwa na watakaogunduliwa, watasimamishwa kazi,wengine nitawafukuza na kuwafikisha mahakamani’’ alisema.
Alisema baadhi ya mameneja wamekuwa wakiharibu sifa ya shirika hilo kwa kuwa wapokeaji wa rushwa kwa kuweka madalali kutafuta wateja wa kupanga katika nyumba za shirika hilo kwa ajili ya makazi na sehemu za biashara.
’’Kama kule Ilala wanaye dalali wao anaitwa Osama, madalali kama hawa wamekuw wakipokea hadi shilingi.
milioni 30 kwa nyumba za biashara na shilingi hadi milioni 8 kwa nyumba za kawaida za makazi, hii ni aibu, njia pekee ni kuitisha tenda na kutoa nyumba hizo kwa utaratibu,’’Alisema Magufuli.
Alisema mameneja hao iwapo watatumia njia bora kupangisha wapangaji wao kwa mujibu wa sheria wataweza kupata fedha nyingi ambazo zitawezesha kuimarisha maslahi ya shirika na hata kufanikiwa kuongezwa mishahara yao.
Alibainisha kuwa mameneja wamekuwa wakilalamikiwa sana kuhusika na rushwa hizo hivyo hawana budi kuacha mara moja mchezo huo kabla ya kuchukuliwa hatua hizo kali za kisheria.
’’Sitaki kuwafukuza watu kazi kama kule ujenzi,sitaki kumfukuza meneja hata mmoja na naahidi nitawalinda kama mtakuwa mnaonewa lakini kwanza mbadilike kuanzia leo,’’ alisisitiza Waziri.