Na Mussa Juma WANANCHI wenye hasira juzi usiku walimuua mtuhumiwa mmoja wa ujambazi kati ya watuhumiwa sita waliokuwa na silaha ambao walimvamia mfanyabiashara maarufu jijini hapa Salim Bayi (45) kwa nia ya kumpora.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Matei Basilio alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 1:30 usiku katika eneo la Majengo Kati katika Manispaa ya Arusha.
Kamanda Basilio alisema katika tukio hilo, mwananchi mmoja Ali Shabani(39) alijeruhiwa vibaya kwa risasi na hadi jana hali yake ilikuwa mbaya na alitarajiwa kuhamishiwa hospitali ya Rufani ya KCMC.
Alisema mara baada ya watu hao kumvamia mfanyabiashara huyo, watu walijitokeza na kuanza kupiga kelele na hivyo kuanza mapambano ya kurushiana risasi na mawe baina ya majambazi na wananchi.
Kamanda alisema katika mapambano hayo, majambazi hao walifanikiwa kukimbia na ndipo mmoja wao alibanwa na wananchi na kupigwa hadi kufariki.
Hata hivyo, kamanda huyo alisema wakati wananchi wakiwa na majeruhiwa wao, Ali Shabani katika hospitali ya Mount Meru walikutana na mmoja wa watuhumiwa hao ambaye naye alifika kutibiwa ambapo walitoa taarifa polisi zilizofanikiwa kukamatwa kwake.
Alisema mtuhumiwa ambaye aliuawa hadi kufikia jana alikuwa bado hajafahamika jina lake na alitoa wito kwa watu kwenda katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya mkoa ya Mount Meru kutamtambua.
Kamanda alisema mtu huyo aliyekamatwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani mara baada ya matibabu ambapo pia hadi jana hakuna silaha ambayo ilikuwa imekamatwa kutokana na tukio hilo.