Na Ally Sonda, Moshi MTUMISHI wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro (KCMC), ameangua kilio mbele ya Katibu Mkuu wa Taifa wa Chama cha Watumishi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE), Ally Kiwenge wakati akiwasilisha kero yake ya kutopewa barua ya kutambuliwa kazini.
Mtumishi huyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Devota, ambaye aliajiriwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii tangu mwaka 1986, alimueleza Katibu Mkuu huyo kuwa katika muda wa miaka 20 sasa, hajapewa barua hiyo hali inayosababisha ajione kama kibarua.
Alitoa lalamiko hilo katikati ya wiki hii, kwenye Mkutano wa Wanachama wa Tughe na Wafanyakazi wa KCMC uliohutubiwa na Katibu Mkuu huyo wakati akiwa katika ziara ya siku mbili mkoani Kilimanjaro.
Alisema pamoja na kutokupewa barua hiyo, Serikali imekuwa ikimkata michango ya pensheni katika mshahara wake, hata hivyo fedha hizo, hafahamu zinakwenda wapi wakati wizara bado haijamtambua kwa barua kama mtumishi wake.
Akizungumza kwenye mkutano huo mara baada ya kukagua ujenzi wa Ofisi ya Tughe,Tawi la KCMC, Kiwenge, alisema ni uonevu na aibu kubwa kwa maafisa waliohusika kumnyima mtumishi huyo barua yake ya kutambuliwa kazini.
Alisema mtumishi yeyote wa serikali anayefanya kazi bila ya kuwa na barua ya kutambuliwa, ajilinganishe na mtu aliyekalia kuti kavu ambalo linaweza kuvunjika wakati wowote na kumjeruhi au kusababisha kifo.
Kiwenge, amemuagiza Katibu wa Tughe Kilimanjaro, John Sanjo, kuorodhesha watumishi wote wa Serikali wakiwamo wa idara za kilimo na mifugo na hospitali ambao hawana barua za kutambuliwa kazini na kuwafikisha majina hayo makao makuu ya chama hicho kwa hatua zaidi.
Hata hivyo, aliupongeza uongozi wa KCMC, kwa kukubali kufungua Tawi la Tughe hospitalini hapo kwa manufaa ya wafanyakazi wake.
Awali katibu Mkuu huyo alifanya kikao na watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ambako alimshauri muajiri wake ambaye kuhakikisha kuwa kamati ya ajira inafanya vikao vyake kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
Alisema madhara ya Kamati hiyo kutofanya vikao ni pamoja na watumishi wengi kutokupandishwa vyeo, kutokurekebishiwa mishahara kwa wale wanaopanda vyeo kama ilivyo kwa watumishi wengi wa Hospitali ya Mkoa ya Mawenzi ambao kwa zaidi ya miaka 15-20 hawajapandishwa vyeo.