UAMUZI kuzuiwa kuapishwa kwa wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki kutoka Kenya, umechukua sura mpya baada ya wakuu wa nchi wanachama kuagiza kupitiwa upya kwa vipengele vya mkataba ulioanzisha mahakama hiyo.
Akijibu maswali ya waandishi wa habari juzi katika Hoteli ya kitalii ya Kibo Palace ya Jijini Arusha, Waziri wa zamani wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Andrew Chenge, alisema kutokana na maelekezo hayo, wanasheria wakuu wa nchi wanachama watakutana Desemba 4, mwaka huu.
Waziri huyo ambaye sasa ni wa Wizara ya Miundombinu, alisema wakuu wa nchi wanachama wamekubaliana kuwa kama yapo matatizo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, hususan mahakama yake, basi nchi wanachama zikae na kuutazama mkataba ulioanzisha jumuiya hiyo na tayari maagizo hayo yanafanyiwa kazi.
“Tumepewa maagizo kuwa tuende tukalitazame hilo ili tuangalie uwezekano wa kufanya marekebisho kwa mambo ambayo hayajakaa vizuri na kwa kuanzia wanasheria wakuu watakutana Desemba 4 kuangalia ni vipengele gani virekebishwe,” alisema Chenge ambaye alishiriki mchakato wa uundaji wa jumuiya na mahakama hiyo, akiwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania.
Alisema kuwa kikao cha wanasheria hao wakuu kitafuatiwa na kikao cha mawaziri wenye dhamana kitakachofanyika Desemba 8, mwaka huu.
Hata hivyo, Chenge alisema, “Suala la mahakama kuzuia kuapishwa kwa wabunge, wenzetu wa Kenya wamelizungumzia kwa kirefu sana na wakapendekeza uamuzi huo utenguliwe, lakini wakuu wa nchi wanachama wameona ni uamuzi halali ambao tukiuingilia tutakuwa tunakiuka dhana ya utawala bora,” alisema.
Chenge aliendelea kufafanua; "Wote tumekubaliana kuwa huo ni uamuzi halali na chombo hiki kinayo mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na lazima utawala bora tuuheshimu na hii itatimiza matakwa ya kuwa na nchi zinazoendeshwa kwa utawala wa sheria.”
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Juma Mwapachu, alisema uamuzi huo wa mahakama hautaathiri au kuchelewesha ustawi wa jumuia hiyo, bali kilichojitokeza ni changamoto kwao, kwani mtoto hawezi kuzaliwa siku hiyo hiyo na akaanza kutembea.
Chenge na Mwapachu ni miongoni mwa viongozi waliokuwa wamefuatana na marais Jakaya Kikwete na Amani Abeid Karume wa Zanzibar katika chakula cha mchana kilichoandaliwa kwa ajili yao katika hoteli ya Kibo Palace na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Wakuu wote wa nchi wanachama walikuwa wapate chakula cha mchana katika hoteli hiyo, lakini kutokana na kuchelewa kumalizika kwa kikao chao na hali ya usalama katika nchi zao waliamua kurejea kwao.
Katika hotuba yake katika mkutano wa wakuu wa nchi wanachama, Rais wa Kenya, Mwai Kibaki, alilalamika kuwa mahakama hiyo ya Afrika Mashariki imeingilia mambo ya ndani ya Kenya.
Comments
Comment #1
(Posted by washawasha) Rating
Mungu endelea kutusikiliza sisi waja wako na kuufanya umoja huo kutokomea na kutokuwepo kabisa.
AMIN