Rais Jakaya Kikwete amesema Serikali haiwezi kuchagua kufundisha masomo ya kawaida tu katika shule bila elimu ya kompyuta kwa sababu taifa litakula hasara katika ulimwengu wa sasa.
Rais Kikwete alisema hayo mjini Zanzibar jana katika ufunguzi wa kituo cha Elimu Mbadala kilichopo Rahaleo kilichojengwa kwa msaada wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
’’Nimearifiwa pia kuwa mbali ya kusoma masomo ya kawaida lakini pia watajifunza elimu ya kompyuta, nawapongeza kwa jambo hili muhimu sana kwani katika ulimwengu wa sasa wa sayansi na teknolojia, kujifunza matumizi ya kompyuta hakuna mbadala,’’ alisema na kuongeza, ’’Ndiyo mwelekeo wa dunia ya leo na ndiyo hali halisi, hatuwezi kuchagua kufanya vinginevyo tutakula hasara.’’
Kituo hicho kitapokea watoto na vijana waliolazimika kukatisha masomo yao kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za umaskini, ndoa na ujauzito, hali ambayo inatoa fursa nyingine kwa vijana kujipatia elimu na kujiendeleza kimaisha.
Aliwasihi vijana watakaopata fursa ya kujiunga na kituo hiki waitumie nafasi hii ipasavyo kwa kuwa hiyo ni nafasi pekee ya kujijengea uwezo wa kujitegemea na kujikomboa kimaisha.
Alisisitiza kuwa katika karne hii ya 21 ambayo imetawaliwa na maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia, hatuna budi kuhakikisha kuwa watoto wanasoma katika mazingira bora yanayovutia kama yaliyopo katika kituo hicho.