Na Daniel Mjema
MVUA za vuli zinazoendelea kunyesha zimeanza kuleta maafa baada ya wananchi zaidi ya 3,000 katika vijiji mbalimbali vya Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, kuzingirwa na maji kutokana na mafuriko.
Vijiji vilivyoathirika ni vile vilivyopo ukanda wa tambarare, ambavyo ni Mandaka, Mnono na Miwaleni ambavyo mwanzoni mwa mwaka huu, vilikumbwa tena na mafuriko na kusababisha kifo cha mtu mmoja aliyesombwa na mafuriko.
Taarifa za awali zilizopatikana jana mjini hapa na kuthibitishwa na viongozi mbalimbali wa serikali, zilidai kuwa nyumba kadhaa zimezungukwa na maji na taathimini ya athari ya mafuriko hayo ilikuwa ikiendelea kufanywa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ngh'oboko, jana aliwathibitishia waandishi wa habari kuwepo kwa mafuriko hayo, lakini akasema hakuwa na taarifa kamili ya athari ya mafuriko hayo.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mussa Samizi, alipoulizwa na waandishi wa habari alionekana kuhamaki na kuhoji taarifa za mafuriko zimewafikiaje waandishi wa habari mapema kiasi hicho.
"Wewe niambie nani amekuambia wakati mimi niko eneo la maafa na hawaniambii, mimi siwajibiki kwa vyombo vya habari kama ni taarifa nitaitoa kwa mkuu wa Mkoa, acheni kunisumbua," alihamaki Samizi.
Hata baada ya waandishi kumsisitizia kuwa suala la maafa kama hilo ni suala linalogusa taifa na linahitaji kutolewa taarifa, bado alishikilia msimamo wake na kumpa simu mtu mwingine ili azungumza na wanahabari.
Wakati Samizi akionekana kukaa mbali na vyombo vya habari, Makamu wa Rais, Dk Ali Mohamed Shein aliwahi kuvisifu kuwa ndivyo vilivyoihabarisha serikali juu ya mafuriko yaliyotokea mwanzoni mwa mwaka huu.
Lakini wakati akitoa taarifa yake kwa Dk Shein, aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Moshi, James oleMillya alitoa lawama nyingi kwa waandishi wa habari kwamba hawakuandika vya kutosha kuhusu mafuriko hayo.