Na Andrew Msechu
AHADI ya Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi na Shirika la Umeme nchini (Tenesco) kuwa kampuni ya Richmond Development ingeongeza megawati 22 za umeme katika gridi ya taifa kabla ya Desemba, imeshindikana.
Ahadi hiyo ni ile aliyoitoa Karamagi katika mazungumzo yake na waandishi wa habari Novemba 23, mwaka huu, kuwa kampuni hiyo ya Richmond ipo katika hatua za mwisho za kufunga mitambo hiyo a mbayo ingeongeza megawati 22 za umeme na kupunguza makali ya umeme kabla ya Desemba inayoanza leo.
Ahadi hiyo pia ilitolewa na Shirika la Umeme nchini (Tanesco) ambalo lilitoa tangazo kwenye vyombo vya habari Novemba 22, mwaka huu na kuahidi kuwa umeme huo wa Richmond ungepatikana kabla ya Desemba.
"Tayari mashine zenye uwezo wa kutoa Megawati 22 za Kampuni ya Richmond Development ya Marekani zimefika nchini na zinatarajiwa kuanza kazi kabla ya mwezi Desemba mwaka huu, na mitambo iliyobaki ya Megawati 80 itafungwa na kuanza kazi kazi kabla ya mwisho wa mwezi Januari 2007," ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco.
Hali hiyo inazidi kupunguza matumaini ya Watanzania juu ya lini hasa mgao wa umeme utapungua, hasa ikizingatiwa kuwa kwa mara kadhaa sasa, ahadi za namna hiyo zimekuwa zikitolewa, lakini hazikamilishwi katika wakati unaotajwa.
Pamoja na utata huo, hakuna mtu aliyekuwa tayari kuulezea, akiwemo, Msemaji wa Tanesco, Meneja Uhusiano, Daniel Mshana, aliyesema kuwa jukumu hilo lipo kwa Richmond ambayo ndiyo inayosimamia masuala ya ufundi.
"Mimi siwezi kuzungumzia suala hilo, kauli aliyoitoa Waziri ndiyo msimamo wa serikali na Tanesco, kuhusu kukamilika kwa matengenezo na kuingia kwa wakati kwa umeme huo kwenye gridi ya taifa inawahusu Richmond, hivyo hao ndiyo wanoweza kuzungumza kuwa wamefikia wapi," alisema.
Juhudi zilizofanywa na gazeti hili kumtafuta Meneja wa Kampuni ya Richmond nchini, Naeem Gire, hazikufanikiwa. Simu yake ya mkononi iliita bila majibu wakati wote, na ofisini kwake walisema yuko kwenye eneo mradi, Ubungo.
Hata hivyo kwenye eneo la mradi juzi walisema hakuwepo na kulikuwepo na tangazo likikataza mtu yeyote kuzungumza na wafanyakazi wa eneo hilo, badala yake wawasialiane na msemaji anayepatikana katika ofisi iliyopo katikati ya Jiji.
Wakati umeme wa Richmond ukiwa bado ni kitendawili, kampuni ya Songas inayozalisha umeme kwa kutumia gesi ya Songosongo, imesema matengenezo ya mtambo namba nne, uliopata hitilafu Oktoba yanatarajiwa kukamilika leo na kuanza rasmi kazi mwisho wa wiki hii.
Mkuu wa kitengo cha Sheria na Masuala ya Jamii wa Songas, Reuben Mwaikinda, aliiambia Mwananchi jana kuwa matengenezo ya mtambo huo yanaendelea vizuri.
Mwaikinda alisema mtambo namba sita uliokodishwa kutoka kwa kampuni ya General Electric (GE) kuziba pengo la mtambo unaofanyiwa matengenezo nchini Uholanzi, nao unaendelea kufanya kazi. "Tunakadiria kuwa mtambo huo uliopelekwa nje utarejea katikati ya Desemba," alisema na kuongeza:
"Kufikia mwisho wa wiki, mitambo yote sita itakuwa ikifanya kazi kwa ukamilifu, hasa baada ya kukamilika kwa matengenezo ya mtambo huu ambao ulikuwa una uwezo wa kuzalisha Megawati 35, ambao tutaendelea kuzalisha kwa ukamilifu," alisema Mwaikinda.
"Pamoja na matatizo ya kiufundi ambayo yamekuwa yakijitokeza, tumejitahidi kuhakikisha kuwa tunayatatua kwa wakati, ili kuhakikisha kuwa tunakamilisha lengo letu la kuzalisha umeme, na tunaendelea kujitahidi kuhakikisha kuwa tunafanya kazi kwa uhakika," aliongeza.
Endapo kweli mitambo hiyo ya Songas itakamilika kufikia Jumapili, kutakuwa na ongezeko la megawati hizo 35, ambazo awali zilidaiwa kuwa kikwazo cha kuonekana kwa megawati 40 zilizoingizwa na kampuni ya Aggreko ya Uarabuni kwenye gridi ya Taifa.