UHARIBIFU mkubwa umefanywa na watu wasiojulikana wanaodaiwa kula njama na kuvunja majengo ya shule mpya ya Sekondari ya Mwaya iliyoko wilayani Kyela mkoani Mbeya na kusababisha masomo kusitishwa.
Mbunge wa Jimbo la Kyela, Dk Harrison Mwakyembe, alisema jana jijini hapa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari akielezea tukio hilo alilodai kuwa ni hujuma na njama za watu wasiopenda maendeleo.
Dk Mwakyembe alisema kuwa uvunjaji huo wa shule iliyojengwa kwa nguvu za wananchi, umeathiri shughuli za kielimu kwenye shule hiyo kwa kuwa vifaa vyote na thamani zilizokuwemo kwenye ofisi za utawala vimeharibiwa na baadhi kuibwa.
Alisema watu hao walivunja madirisha, milango na walipoingia ndani waliendelea kuvunja kuta kwa kutumia vitu vyenye ncha kama vile shoka,nyundo na nyundo na kuvunja vunja samani za ofisi zilizokuwepo.
Mbunge huyo alisema, kamati ya shule hiyo kwa kushirikiana na wahandisi walifanya tathimini ya haraka na kugundua kuwa mali yenye thamani Sh5 milioni imeharibiwa na nyingine kuibwa.
Alisema kuwa tukio hilo sio la kwa kuwa wiki mbili zilizopita uvamizi kama huo ulifanyika kwenye shule hiyo kwa kuvunja makenchi kwenye vyoo vya wanafunzi na mabati kung'olewa ukiwemo msingi wa nyumba za walimu uliovunjwa kisha wahusika hao kutoweka.
Katika Mkutano na wakazi wa Mwaya aliwataka wawafichue waliohusika na njama hizo kwa kuwa wanawafahamu na wanaishi nao. Aliwataka watoe taarifa polisi ili waweze kunaswa vinginevyo uharibifu huo utakwamisha masomo kwa watoto wao.
Wakati wananchi wanatafakari hatima ya hujuma hiyo, mlinzi wa shule hiyo na wanakijiji wawili wanashikiliwa na polisi kuhusiana na tukio hilo.