Na Ally Sonda
MUASISI wa Chama cha Tanganyika African National Union (TANU) na Chama Cha Mapinduzi (CCM), amemtaka Rais Jakaya Kikwete kufuata nyayo za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutangaza majina ya watu wanaodhaniwa kuwa ni wafanyabiashara wa dawa za kulevya nchini.
Mzee Bomba, mkazi wa Mabogini, alionya kuwa licha ya Rais Kikwete kupendwa na watanzania wengi, serikali yake inaweza kuonekana ya ajabu endapo haitawataja na kuwafikisha mahakamani wanaotuhumiwa kufanya biashara hiyo haramu.
Bomba ambaye aliwahi kuwa dereva wa Waingereza wakati wa vita kuu ya Pili ya Dunia, alisema kutotajwa kwa majina ya wafanyabiashara hao na kuwafikisha mahakamani unawapa mashaka makubwa wananchi.
Alisema visingizio vinavyotolewa na vyombo vya dola likiwamo Jeshi la Polisi kuwa linafanyia kazi majina ya wafanyabiashara hao, hazina msingi kwa kuwa watu hao walipaswa kufanyiwa uchunguzi wakiwa mbaroni.
" Polisi wakisikia mtu fulani anauza bangi wanavamia nyumba yake na kumkamata na hata wakipekuwa nyumba na wakakosa hiyo bangi bado watamchukua hadi kituoni na kumsweka rumande ... sasa mbona hao wanaouza dawa hawaswekwi rumande? " alihoji.
Alisisitiza kuwa, sheria inayotumika kuwabana wauza mirungi, bangi na gongo isitumike kwa wanyonge bali iwaadhibu wakosaji wote ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .
Amempongeza Mbunge wa Viti Maalum (Vijana-CCM), Amina Chifupa Mpakanjia kwa ujasiri wa kuamua kulisaidia Jeshi la Polisi kuwanasa wauza unga na kumuomba Kikwete kumlinda baada ya kuonyesha kukerwa na vitendo hivyo.