Irene Lipende
RAIS wa Burundi, Piere Nkurunzinza amevutiwa na shughuli zinazofanywa na Shirika la Uchumi la Jeshi la Kujenga Taifa nchini(SUMA-JKT) na kuahidi kuleta wanajeshi wake kupata mafunzo.
Nkurunzinza alisema hayo jana Jijini Dar es Salaam, alipotembelea JKT kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na jeshi hilo.
"Nawashukuru Watanzania kwa ukarimu wenu na uvumilivu mkumbwa mliouonyesha kwa muda wote ambao wakimbizi wa Burundi waliishi nchini kwenu na ninaahida kwamba, ili kudumisha umoja wetu, nitawaleta wanajeshi wangu waje kupata mafunzo Tanzania," alisema Nkurunzinza.
Akiongozwa Mkuu wa JKT, Meja Jenerali Abdulrahman Shimbo, Nkurunzinza alitembelea Kiwanda cha Kutengeneza Dawa za Binadamu (Tanzansino) kinachomilikiwa na jeshi kwa ushirikiano na Serikali ya China.
Kiwanda hicho kimefanikiwa kutengeneza dawa mbalimbali na kufanikiwa kuzindua dawa mpya ya malaria, iitwayo Dihydrotan.
Pia alitembelea Kiwanda cha Nguo cha Camisuma ambacho kipo chini ya SUMA-JKT ikishirikiana na serikali ya Bulgaria, kujionea baadhi ya shughuli zinzofanywa kiwandani humo.
Meneja wa kiwanda hicho, Ofelia Tonog, alimuomba rais huyo apeleke aagizo ya kushonewa nguo za jeshi lake katika kiwanda hicho, ambacho kinatengeneza nguo za askari wa JKT.
Kiwanda hicho ambacho kilianzishwa April mwaka huu kimeshatoa ajira kwa vijana 231, ambapo kati yao 172 ni wanawake na 59 ni wanaume na mpaka sasa kimeshatengeneza jozi 30,000, kati ya hizo 8,443 ni sare za wafungwa.