Na Lilian Lugakingira
WAKAZI wa Kijiji cha Bugango Kata Kakunyu wilayani Missenye, wamekataa kuongozwa na mwenyekiti wao, Sofia Mbani kwa madai kuwa, anaishi nchini Uganda badala ya Tanzania.
Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti wakazi hao walidai kuwa, tangu achaguliwe mwaka juzi kuwa mwenyekiti wa kijiji hicho, amekuwa akiishi nchini humo.
Kutokana na kijiji hicho kuwa mpakani mwa Tanzania na Uganda, wakazi hao wamedai mwenyekiti huyo amekuwa akilala nchini humo na kuja kazini katika ofisi ya kijiji asubuhi na jioni kurejea nyumbani kwake.
Waliendelea kudai kuwa, kutokana na hali hiyo hawawezi kuendelea kuongozwa na mwenyekiti huyo badala yake, wanaomba ridhaa ya kuchagua mwingine.
Akizungumzia madai hayo, mwenyekiti huyo alisema kuwa anaisi kuwa huenda wakazi hao hawamtaki baada ya kusambaa kwa kwa taarifa kuwa ameshirikiana na uongozi wa Ranchi ya Missenye kuwanyang’anya ardhi yao .
Naye Katibu Tarafa wa Missenye Abas Ngilwa, alisema mwanzoni mwenyekiti huyo, alikuwa akiishi Tanzania, lakini kutokana na marekebisho ya mpaka mpya kati ya Tanzania na Uganda yaliyofanyika mwishoni mwa mwaka 2003, shamba na nyumba yake vilirudi nchini humo .
Kwa mujibu wa Ngilwa, baada ya kuzuka kwa malalamiko kuhusiana na mwenyekiti huyo kuishi Uganda, alilazimika kutafuta nyumba ya kupanga kijijini hapo ambako hadi sasa anaishi.
Mwenyekiti huyo alichaguliwa na wakazi hao kushika wadhifa huo wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika mwaka juzi.