Na Daniel Mjema, Moshi
MFANYAKAZI wa Kitanzania katika kampuni ya China ya Sietco, Michael Jacob, amefungua kesi ya madai mahakamani dhidi ya viongozi watatu wa kampuni hiyo, akiwadai fidia ya Sh50 milioni kwa kumpiga akiwa kituo cha polisi.
Wanaodaiwa fidia hiyo ni raia wa China, Zhang Te Cheng, Zhang Ming Xiang na Hnang Gem, ambao nao wamemgeuzia kibao Jacob na kumdai fidia ya Sh80milioni.
Katika hati ya madai aliyoiwasilisha Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini hapa, Jacob anadai fidia hiyo kutokana na kipigo alichokipata kutoka kwa Wachina hao akiwa ndani ya kituo cha Polisi Tarakea wilayani Rombo.
Jacob analalamika kuwa Oktoba 15 mwaka huu, wakiwa ni nia ovu, raia hao wa Kichina walimshambulia kwa kumpiga, wakimtuhumu kuiba mafuta madai ambayo anasema hayakuwa na ukweli wowote.
Analalamika kuwa licha ya kukimbilia katika kituo cha polisi kuomba msaada, Wachina hao walimfuata na kumshambulia na kumsababishia madhara kichwani na sehemu mbalimbali za mwili wake.
"Walinishambulia kwa madai hayo huku wakijua kuwa yalikuwa ni ya uongo na licha ya kunijeruhi na kunisababishia madhara mwilini, lakini pia walinidhalilisha utu wangu," anadai Jacob katika hati hiyo.
Jacob amefafanua kuwa baadaye Wachina hao walikamatwa na kufunguliwa mashitaka ya jinai na walikiri makosa yao na kupigwa faini pamoja na fidia inayofikia jumla ya Sh200,000.
Hivyo, Jacob anaiomba mahakama iwaamuru Wachina hao na kampuni ya Sietco, kumlipa Sh25 milioni kwa ajili ya madhara ya mwili aliyoyapata na Sh25 milioni nyingine kwa kumchafua jina lake.
Lakini wachina hao kupitia kwa wakili wao, Alfonce Urio, wa mjini hapa, wamekanusha madai hayo na kuwasilisha madai mbadala ya Sh80 milioni, wakidai kuwa wao ndio waliostahili kufidiwa kwa matendo ya Jacob.
Katika hati yao ya majibu waliyoiwasilisha mahakamani, Wachina hao wanadai kutokana na kipimo cha mafuta, Sietco na uongozi mzima walikuwa na sababu ya kuamini kulikuwa na matumizi ya mafuta yasiyo ya kawaida.
Kesi hiyo inayovuta hisia za watu kutokana na tukio lenyewe lilivyokuwa, imepangwa kutajwa kwa mara ya kwanza leo mbele ya Hakimu Mkazi, Janet Masesa wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi.