Na Salhim Shao
MGAMBO wa Jiji la Dar es Salaam, wameomba waruhusiwe kutumia mabomu ya machozi katika zoezi la kuwaondoa wamachinga mitaani.
Wakizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Patrick Tsere jana, mgambo hao walisema walimuomba Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, awaruhusu kutumia mabomu ya machozi wakati wakipambana na wamachinga.
"Tunapokwenda kufanya kazi ya kuwaondoa maeneo kama ya Kariakoo tunazingirwa na raia na kulazimika kuacha kazi hiyo kwa kushindwa kuwatawanya," alisema Damiani Mpangala, mmoja wa mgambo hao wa Manispaa ya Ilala.
Mgambo hao wa jiji walisema wanaposhambuliwa au kuzuiwa kufanya kazi zao na raia wenye hasira, hulazimika kuondoka kwani iwapo watatumia silaha za moto wanazopewa, madhara yake yanaweza kuwa makubwa.
Pia walilalamikia tabia ya viongozi wa serikali ambao wamekuwa wakiwaingilia pindi wanapowakamata watuhumiwa. "Tunakamata mtu baadaye anakuja kiongozi na kutaka tumwachie wakati amevunja sheria, inaumiza sana," alisema.
Walitolea mfano katika operesheni waliyokuwa wakifanya ya kuondoa vibanda katika maeneo ya jiji, ambako baadhi ya viongozi wamekuwa wakiwataka waache baadhi ya vibanda na kuwaonyesha vingine vya kubomoa.
"Suala hili limefanya tuonekane tunafanya kazi kwa upendeleo na hivyo kujengewa chuki na watu, tunataka kama tunafanya kazi tusiangalie sura, vinginevyo hata heshima ya serikali inapungua kwa watu," alisema mgambo mwingine, Khalfan Kimaro.
Mkuu wa wilaya ambaye alikuwa amemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro katika mkutano huo, alisema amepokea masuala yote waliyomweleza na kuwa atafikisha kwa watekelezaji ili yafanyiwe kazi.